Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Monday, January 11, 2016

WAKULIMA WA MPUNGA IGUNGA WATAKIWA KUACHA KILIMO CHA MAZOEA




Na lucas Raphael,Igunga.

Wakulima wa zao la mpunga katika skim ya Umwagiliaji Mwamapuli wilayani Igunga mkoani Tabora wametakiwa kuachana na kilimo cha mazoea na badala yake wawe na mpango kazi  ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo.

Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa wilaya ya Igunga Ziporra Pangani  baada ya kituo cha utafiti wa kilimo cha Tumbi katika manispaa ya Tabora kutoa mafunzo ya kilimo shadidi kitakachoongeza kipato na uzalishaji kwa wakulima hao.

Amesema skim hiyo ni kubwa kwa kanda ya Magharibi hivyo wakulima hao hawana budi kuzingatia mafunzo waliyopewa ya kilimo shadidi ambacho kitawaletea mafanikio makubwa.

''Wakulima napenda kuwaasa kuwa baada ya kupata  mafunzo sasa mbadilike msilime kilimo cha mazoea limeni shadidi mtakuwa matajiri wakubwa hasa wa mpunga kwani kilimo ndio kila kitu.'' amesema mkuu huyo wa  wilaya.

Aidha Pangani ametahadharisha kuwa miradi mingi imekuwa ikipotea baada ya wafadhili kuhitimisha ufadhili wao na kusisitiza kuwa mradi huo unapaswa kuwa endelevu kwa wakulima hao hata baada ya kuhitimishwa kwa ufadhili.

Mtafiti wa mazao ya mpunga Dkt. Tulole Lugendo amesema  mradi huo utakuwa endelevu kwa kuwa umemgusa mkulima mmoja mmoja na kuongeza kuwa kituo hicho kitaufuatilia kuona namna wakulima hao wanavyozingatia mafunzo hayo.

Mtafiti huyo amesema wakulima walionufaika na mafunzo hayo ni zaidi ya 20 huku skim hiyo ikiwa na wakulima zaidi ya 900 na kuongeza kuwa wakulima hao watakuwa walimu kwa wakulima wengine.

Mwenyekiti wa ushirika wa Mwamapuli Robert Lufunga amekipongeza kituo hicho cha utafiti kwa kutoa mafunzo hayo ambayo yatanufaisha wakulima hao kwa kuongeza tija na hivyo kupambana na umasikini.

Mafunzo hayo yalifanyika kwenye ukumbi wa Sakao mjini Igunga na  kufadhiliwa na serikali ya Japan na kuendeshwa na kituo cha utafiti wa kilimo Tumbi kinachohudumia kanda ya Magharibi.

No comments: