Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Monday, January 25, 2016

TAARIFA YA MAPATO NA MATUMIZI YA SHULE YA MSINGI ISHIHIMULWA YAKATALIWA NA WANANCHI



Na Paul Christian, Uyui.

Wakazi wa kijiji cha Ishihimulwa kata ya Bukumbi wilaya ya Uyui mkoani Tabora wameikataa taarifa ya idara ya elimu waliyosomewa kwenye mkutano mkuu wa kijiji hicho.

Wakazi hao wamesema idara ya elimu yenye shule ya msingi Ishihimulwa imeeleza kuwa na mapato ya shilingi 90,000/- kwa mwaka jambo ambalo haliendani na uhalisia wa mapato ya shule hiyo.

Akisoma taarifa hiyo ya mapato na matumizi afisa mtendaji wa kijiji hicho Jiji Numbu amesema shule hiyo kwa mwaka ulioisha ilikuwa na mapato hayo jambo ambalo lilipingwa vikali na wakazi hao.

Wakazi hao wameutupia lawama uongozi wa shule hiyo ya msingi kwa kutumia vibaya na kuficha hesabu halisi ya fedha za mapato ya shule hiyo ambayo imekodisha eneo la mnara wa kampuni ya Airtel kwa shilingi milioni moja na laki sita kwa mwaka iweje leo mapato yawe shilingi 90,000/- kwa mwaka.

Wamevitaja vyanzo vingine vya mapato katika shule hiyo kuwa ni ruzuku ya shilingi 124,000/- kwa mwaka, ukodishaji wa matela ya kukokotwa na ng’ombe ambapo tela moja ukodishwa kwa shilingi 1,000/- na wakati huu wa masika ukodishwa kwa wastani wa mara 15 kwa siku na kipindi cha kiangazi ni wastani wa mara 32 kwa siku.

Kutokana na hali hiyo diwani wa kata ya Bukumbi John Majala ameiagiza kamati ya shule hiyo kuandaa na kuwasilisha hesabu za mapato na matumizi ndani ya siku 14 ili wananchi waipate na kujiridhisha.

No comments: