Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, January 20, 2016

MTEMI MILAMBO KIOO CHA HISTORIA YA TABORA

PAROKIA YA KANISA KATOLIKI ULYANKULU


Na Paul Christian, Ulyankulu.

Mtemi Milambo aliyeishi zaidi ya miaka 132 iliyopita anaelezwa kuwa miongoni mwa waafrika wachachewa wakati huo walitumia choo.

Akizungumzia mambo ya kihistoria yaliyopo hivi sasa katika tarafa ya Ulyankulu wilaya ya Kaliua mkoani Tabora diwani wa kata ya Uyowa Alphonce Msanzya amesema hadi leo hii shimo pamoja na miti iliyokuwa ikitumiwa kwenye choo hicho vipo.

Diwani huyo ameeleza kuwa hali hiyo inamaanisha mtemi Milambo alikuwa mtu aliyestaarabika na upeo mkubwa wa kutambua na kufahamu mambo mbalimbali ya mahusiano, utawala,ulinzi na matumizi ya zana bora.

Msanzya amesema, “katika kitongoji cha Itambilo, kijiji cha Songambele kata ya Uyowa kuna mti aina ya “Mhama” ambao ulitumiwa na askari wa mtemi Milambo waliojulikana kama “walugaluga” kwa ajili ya kufanya mazoezi ya kulenga shabaha kwa kutumia bunduki.”

Diwani huyo anafafanua kuwa mti huo hadi leo upo katika eneo hilo na unazo alama za matundu ya risasi na hivyo kudhihirisha kuwa mtemi huyo alitumia zana mbalimbali kutoka nje ya eneo lake la kiutawala.

Amesema jambo lingine la kihistoria lililopo kwenye tarafa hiyo ni katika eneo la barabara ya kutoka Ulyankulu kuelekea Kahama maarufu kama barabara ya sita ambapo limewekwa karavati.

Msanzya amebainisha kuwa karavati hilo limewekwa hapo kutokana na kuwepo kwa handaki lililochimbwa na askari wa mtemi Milambo “walugaluga” wakati akijiandaa kumshambulia mjomba wake.
Amefafanua kuwa lengo la mtemi Milambo lilikuwa ni kuyafikia makazi ya mjomba wake kwa kupitia handaki na kisha kumshambulia lakini kitendo hicho hakikumfurahisha mama yake mzazi  Milambo ambaye kwa wakati huo alikuwa akiishi kwa kaka yake ambaye ndiye huyo mjomba wake na mtemi Milambo.
Msanzya ameeleza kuwa wazee wa maeneo hayo wanasema kuwa mtemi Milambo alifanikiwa kuchimba handaki hilo na kuyakaribia makazi ya mjomba wake kwa lengo la kufanya shambulio.
“Lakini siku moja akiwa kwenye harakati hizo mtemi Milambo aliletewa ugali ambao inasemekana kwa mazingara ulibadilishwa na kupewa ugali wenye sumu ambapo aliula na kuanza kuugua kwenye mfumo wa chakula kuanzia mdomoni, kwenye koo hadi tumboni.
Msanzya amesema na hiyo ndio sababu Padri mmoja aliwahi kuandika kuwa mtemi Milambo alikufa kwa kansa ya koo.
Diwani huyo ametaja eneo linguine lilibaki na kumbukumbu ya kihistoria ni eneo ambalo Parokia ya kanisa Katoliki Ulyankulu limejengwa kwa kuwa lilikuwa ni ngome ya ikulu ya mtemi Milambo.
ENEO LILILOCHIMBWA HANDAKI
“Eneo hilo lilizungukwa na handaki lililochimbwa na “walugaluga” kwa ajili ya kuimarisha ulinzi na wakati likichimbwa handaki hilo walilifanyia majaribio ya kuwasukumia watu na walipokufa iliwahakikishia kuwa handaki hilo liko tayari kwa ulinzi.” Amesema kiongozi huyo.

 Amesema kitu kingine cha kusisimua katika eneo hilo ni kaburi la mtemi Milambo lililopo kwenye kitongoji cha Ikonongo ambapo pia kuna kifusi kikubwa cha nyumba aliyokuwa akiishi mtemi huyo mashuhuri.
Msanzya amebainisha kuwa  katika eneo hilo kuna makaburi ya watemi waliotawala kabla na baada ya mtemi Milambo.
Amesema hata kiti alichokuwa akikitumia mtemi Milambo wakati wa shughuli zake mbalimbali zikiwemo za kiutawala ukifika huko utakikuta hadi leo kipo.
Diwani huyo wa kata ya Uyowa amesema kwa ujumla mkoa wa Tabora umejaliwa kuwa na historia ya kipekee jambo muhimu linalopaswa kufanywa ni kuutangaza utajiri wa kihistoria uliopo ili uanze kuwanufaisha watu wetu.

No comments: