Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Thursday, January 14, 2016

KAULI YA “WATU WANGU, WATU WANGU,” INACHANGIA KUHARIBU MAZINGIRA.

MKUU WA WILAYA YA TABORA SULEIMAN KUMCHAYA AKIWAHUTUBIA MADIWANI WA HALMASHAURI YA MANISPAA YA TABORA WAKATI WA UFUNGUZI WA SEMINA YA UPATIKANAJI WA MAJI KATIKA MANISPAA HIYO

Na Paul Christian, Tabora.
 
Madiwani wa halmashauri ya Manispaa ya Tabora wameagizwa kuongoza mapambano dhidi ya uharibifu wa mazingira katika maeneo ili kulinda uoto wa asili unaosababisha maji, mvua, rutuba na kuongeza mazao ya chakula na biashara.

Agizo hilo limetolewa leo na mkuu wa wilaya ya Tabora Suleiman Kumchaya wakati akifungua semina ya siku moja iliyohusu hali ya upatikanaji wa maji katika manispaa hiyo iliyoandaliwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira TUWASA  na kufanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Mamlaka hiyo.

Amesema wananchi wanahatarisha  vyanzo vya maji kwa kukata miti, kuchungia mifugo na hata kufyeka misitu kwa shughuli za ufugaji,biashara kilimo, na makazi  hali inayopaswa kupigwa vita kwa nguvu zote.

Kumchaya amebainisha kuwa bwawa la Igombe linalotegemewa kama chanzo cha maji kwa wakazi wa mji wa Tabora liko kwenye hatari ya kukauka endapo viongozi na wananchi hawatachukua hatua za makusudi kulinda mazingira ya vyanzo vya maji.

Aidha mkuu huyo wa wilaya amewanyooshea kidole wanasiasa kuacha tabia ya kuwatetea wananchi wanaovamia maeneo yaliyotengwa au kuharibu mazingira kwa makusudi kwa madai ya kuwa wahusika ni wapiga kura wao.

Kumchaya amewataka madiwani hao kutumia kamati zao za maendeleo ya kata  kujadili na kupanga mambo ya maendeleo ikiwemo kulinda na kuhifadhi mazingira katika maeneo yao.

Amewasisitiza madiwani hao kuwa na ratiba endelevu ya kutembelea, kusimamia,kukagua na kuwaelimisha wananchi wao juu ya umuhimu wa kutunza mazingira.

Mkuu huyo wa wilaya amesema athari za uharibifu wa mazingira katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Tabora zimeanza kuonekana kutokana na mvua kupungua ukilinganisha na miaka ya nyuma.

No comments: