Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Friday, January 8, 2016

AFISA TARAFA AAGIZA SERIKALI ZA VIJIJI KUANDAA REJISTA YA WAKAZI



Na Paul Christian, Ulyankulu.

Halmashauri za serikali za vijiji katika jimbo la Ulyankulu wilaya Kaliua mkoani Tabora wameagizwa kuwa na orodha ya wakazi (rejista) katika maeneo yao ili kuwatambua wageni wanaoingia kwenye vijiji hivyo.

Agizo hilo limetolewa na afisa tarafa wa Ulyankulu John Chitanda alipokuwa akizungumza kwenye kikao kilichowakutanisha wenyeviti wa vitongoji na vijiji, maofisa ugani, watumishi wa afya,walimu wakuu na wakuu wa shule katika ukumbi wa mikutano wa kanisa katoliki barabara ya 13.

Amesema orodha ya wakazi katika vijiji itasaidia kuwatambua wageni na hivyo kudhibiti uhalifu, uingizaji wa mifugo, uhifadhi wa mazingira na upangaji wa matumizi bora ya ardhi.

Chitanda amebainisha kuwa utaratibu huo ulikuwepo huko nyuma na ulisaidia kuwatambua wageni na hivyo kudhibiti uhalifu katika vijiji hivyo.
Afisa tarafa huyo amesema tarafa ya Ulyankulu inapakana na hifadhi za mapori ya akiba ambayo yamekuwa yakivamiwa na mifugo inayotoka nje ya tarafa hiyo huku viongozi wa serikali za vijiji wakidai hawana taarifa kuhusu wamiliki wa mifugo hiyo.

Chitanda amesema kitendo hicho huenda kinafanywa kwa makusudi na viongozi hao kwa kuwa wanapokea rushwa kutoka kwa wafugaji ili waingize mifugo ambayo inazidi uwezo wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya marisho na maji jambo linalosababisha waingie kwenye maeneo ya hifadhi.

Amewashauri viongozi wa serikali za vijiji kutojiamulia kupokea mifugo pasipo kuhusisha wananchi kupitia mikutano mikuu ya vijiji kulingana na uwezo wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili hiyo ili kuepusha migogoro baina ya wafugaji na wakulima au wafugaji na maofisa wa uhifadhi wa mapori ya akiba.

Aidha afisa tarafa huyo amehimiza kufanya ziara ya kushitukiza kukagua rejista hiyo ya wakazi na namna inavyotumika kuorodhesha wakazi wote waliopo kwenye vijiji na watakao bainika kutotekeleza agizo hilo watachukuliwa hatua za kinidhamu.



No comments: