Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, January 20, 2016

HALMASHAURI ZIWEKEZE KWENYE KILIMO CHA UMWAGILIAJI



 
MAJI YA MVUA ENEO LA IGANGE MANISPAA YA TABORA
Na Paul Christian, Tabora

Halmashauri ya Manispaa na wilaya mkoani Tabora zimeshauriwa  kuwekeza kwenye miradi ya kuvuna maji ya mvua ikiwa ni pamoja na kuchimba mabwawa yatakayo tumika kwa kilimo cha umwagiliaji ambacho kitazalisha ajira kwa vijana na akinamama.

Ushauri huo umetolewa na katibu wa siasa, itikadi na uenezi wa Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Uyui Said Katala alipofanya mahojiano maalum na Tabora Watch kuhusu mbinu za kukabiliana na tatizo la ajira mkoani Tabora.

Amesema endapo halmashauri zitaibua miradi ya kuchimba mabwawa, kujenga mabanio ya kukinga maji na mifereji katika maeneo ya mabonde itasaidia kuinua shughuli za kilimo cha mazao ya chakula na biashara.

Katala amesema kuibua, kusimamia na kuendeleza miradi kama hiyo katika kilimo itasaidia kutoa ajira kwa watu wengi kwa wakati mmoja.

Aidha ameeleza kuwa wakazi wa maeneo mengi katika mkoa wa Tabora huwa wanakumbwa  na njaa mara kwa mara na ili kukabiliana na tatizo hilo halmashauri ziwekeze kwenye kilimo cha umwagiliaji.

SAID KATALA
Katala amesema wakati umefika kwa wataalam kutumia elimu zao kuisaidia jamii kuondokana na umasikini, ukosefu wa ajira na baa la njaa kwa kuwekeza katika uvunaji wa maji ya mvua.

Katibu huyo muenezi amesema katika msimu huu wa mvua sehemu kubwa ya mkoa wa Tabora imepata mvua nyingi ambayo maji yake yanapotea bure na wakati mwingine kuleta madhara kwenye mashamba na makazi ya wananchi.

Amesema uvunaji wa maji hayo ni jambo linalopaswa kuangaliwa kwa umakini wa kipekee kwa lengo la kukuza uchumi wa mkoa wa Tabora.

No comments: