Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Friday, January 15, 2016

SEHEMU YA PILI: TUNAJIFUNZA NINI KWA TUKIO HILI LA KIHISTORIA- OPERESHENI ENTEBBE



.................Tulipoishia sehemu ya kwanza ya simulizi hii ya kihistoria watekaji wakaongeza siku za mazungumzo na kwamba siku ya mwisho ya utekelezaji wa madai yao ikawa majira ya mchana ya tarehe 4 Julai, 1976. Sasa endelea.....................
MAKOMANDOO WA ISRAEL

Paul Christian, Tabora.

OPERESHENI ENTEBBE

Siku hiyo hiyo ya Tarehe 1 Julai, 1976 kwa mara nyingine Watekaji waliwaachia huru mateka wengine 100 wasiokuwa raia wa Israel ambao walisafirishwa kuelekea Paris, Ufaransa.

Mateka 106 waliendelea kushikiliwa wakiwemo wafanyakazi 12 wa ndege hiyo ya Air France 139, 10 wakiwa vijana Wakifaransa na 84 Raia wa Israel au wenye asili ya Israel.
 
Serikali ya Israel ilijaribu mara kadhaa kufanya majadiliano ya kisiasa ili mateka hao waachiliwe huru.

Hata hivyo baraza la mawaziri la Israel lilikuwa limejiandaa kuwaachia huru wafungwa wakipalestina wapatao 40 endapo ufumbuzi wa kijeshi usingeonekana kufanikiwa.

Afisa mstaafu wa Jeshi la Israel IDF Baruch “Burka” Bar Lev alikuwa akifahamiana na Idd Amin kwa miaka mingi na alidhaniwa kuwa na uhusiano wa kibinafsi na kiongozi huyo wa Uganda. 

Kwa maombi ya baraza la mawaziri la Israel afisa huyo alifanya mazungumzo kwa njia ya simu mara kadhaa na  Idd Amin ili kujaribu kufikia muafaka wa kuachiliwa huru  kwa mateka hao lakini hakufanikiwa.

Serikali ya Israel iliiomba serikali ya Marekani imshawishi Rais wa Misri Anwar Sadat azungumze na Idd Amin kwa ajili ya kuachiliwa huru kwa mateka wa Israel.

Siku ile ya Julai 1, 1976 serikali ya Israel iliomba ipewe muda zaidi wa mazungumzo, na watekaji kutoa siku ya mwisho kuwa tarehe 4 Julai 1976, Rais wa Uganda Idd Amin aliwashawishi watekaji hao  kukubaliana na ombi la Israel.

Idd Amin alifanya hivyo kwa kuwa alikuwa na safari ya kidplomasia  kuelekea Port Louis nchini Mauritius ambapo angekabidhi uenyekiti wa Umoja wa nchi za Afrika OAU kwa Seewoosagur Ramgoolam.

Kuongezwa kwa muda wa mwisho hadi Julai 4, 1976 kulitoa fursa kwa jeshi la Israel kuvamia Entebbe.

Mnamo tarehe 3 Julai, 1976 majira ya saa 12:30 jioni Baraza la Mawaziri la Israel liliridhia mpango wa jeshi la nchi hiyo kwenda kuwakomboa mateka wa Israel katika ardhi ya Uganda.

Mpango wa uvamizi uliwasilishwa kwenye baraza hilo na Meja Jenerali Yekutiel “Kuti” Adam pamoja na Brigedia Jenerali Dan Shomron.
Brigedia Jenerali Shomron aliteuliwa kuwa kamanda wa opereseni hiyo ya kijeshi.

Licha ya mpango huo wa siri wa serikali ya Israel,  Rais wa Misri Anwar Sadat alijaribu kufanya mazungumzo na uongozi wa Chama cha Ukombozi wa Wapalestina PLO pamoja na serikali ya Uganda.

Mwenyekiti wa PLO Yesser Arafat alimtuma mjumbe wake Hani al-Hassan kwenda Uganda kuzungumza na watekaji pamoja na Rais wa nchi hiyo Idd Amin, hata hivyo watekaji hao wa kundi la PFLP-EO walikataa kuonana na mjumbe huyo wa Arafat.

Baada ya serikali ya Israel kushindwa kupata ufumbuzi wa kisiasa dhidi ya madai ya Watekaji ili wawachilie huru mateka waliokuwa wakiwashikilia, serikali hiyo iliamua kutumia mbinu za kijeshi. 

Luteni Kanali Joshua Shani, alipewa usukani wa kuongoza operesheni hiyo ambapo mwanzoni jeshi la Israeli lilipanga kudondosha makomandoo ziwa Victoria na kisha kutumia boti  zilizotengenezwa kwa plastic kuelekea kwenye Uwanja wa Ndege wa Entebbe ulioko kando ya ziwa hilo.

Kwenye mpango huo walipanga kuwaua watekaji na kuwakomboa mateka wote na baadae kumuomba Rais wa Uganda Idd Amin njia ya kuondoka kuelekea Israel.

Hata hivyo mpango huo wa awali ulifutwa kwa sababu  ulihitaji muda mwingi na jeshi halikuwa na muda wa kutosha, na pia uwepo wa mamba kwenye ziwa Victoria.

Aidha jeshi la Israel  katika uvamizi huo lilifikiria mahali pa kutua na kujaza mafuta ndege zake aina ya Lockheed C-130 Hercules  ambazo zilipangwa kutumika kwenye uvamizi huo wa Entebbe, Uganda.

Hiyo ilikuwa changamoto kwa jeshi la Israel kwa kuwa walihitaji msaada kutoka kwenye moja ya nchi za Afrika Mashariki na hususani Kenya.

Mataifa ya Afrika Mashariki hayakuwa tayari kuujingiza kwenye mgogoro na Idd Amin au Wapalestina kwa kuisaidia Israel kutumia viwanja vya ndege ndani ya mipaka ya nchi hizo.

Jeshi la Israel lilitambua lisingeendelea na mpango wake pasipo kupata msaada wa nchi mojawapo ya Afrika ya Mashariki. 

Mmiliki wa hotel maarufu za Block hotels chain nchini Kenya na raia wa Israel akishirikiana na wenzake wenye asili ya Israel jijini Nairobi walitumia ushawishi wa kisiasa na kiuchumi kumshawishi Rais wa Kenya Mzee Jomo Kenyatta kuisaidia Israel.

Hatimaye Israel ikapewa ruhusa kutoka serikali ya Kenya kwa ajili ya jeshi lake kutumia anga na kujaza mafuta kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta jijini Nairobi.

Aidha Waziri wa kilimo wa Kenya Bruce McKenzie alimshawishi Rais Kenyatta kuliruhusu shirika la kijasusi la Israel Mossad kukusanya taarifa muhimu kabla ya jeshi la Israel kuvamia Entebbe.

Shirika hilo la kijasusi la Israel lilitoa picha kamili ya mahali walipo mateka, idadi ya watekaji, silaha walizonazo watekaji na namna jeshi la Uganda lilivyojihusisha na mgogoro huo.

Mossad ilipata taarifa za kijasusi kutoka kwa mateka wasio waisrael ambao walioachiwa huru na kusafirishwa hadi Paris nchini Ufaransa.

Shirika hilo pia lilitumia taarifa za makampuni ya ujenzi ya nchini Israel ambayo yalishiriki katika ujenzi wa majengo mbalimbali barani Afrika katika miaka ya 60 na 70.

Mossad  iliwasiliana na kampuni kubwa ya ujenzi nchini humo Solel Boneh ambayo ilijenga jengo ambalo mateka wenye asili ya Israel walikuwa wakishikiliwa kwenye uwanja wa Entebbe nchini Uganda.

Wakati wakipanga kutekeleza operesheni hiyo, jeshi la Israel likisaidiwa na raia wa nchi hiyo walioshiriki kujenga jengo la Entebbe, lilijenga jengo la muda la mfano lililofanana na lile la Entebbe lililokuwa na mateka.

.................Usikose sehemu ya tatu ya simulizi hii ya kusisimua

No comments: