Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, January 10, 2016

MTO IGOMBE UKO KWENYE HATARI YA KUTOWEKA



Na Paul Christian, Ulyankulu.

Mto Igombe uko kwenye hatari ya kutoweka kutokana na vitendo vya uharibifu wa mazingira.

Afisa mhifadhi wanyamapori wa pori la akiba la Kigosi Moyowosi kanda ya Kusini mkoani Tabora Thomas Mgeta Jumbula ametoa maelezo hayo wakati wa kikao cha kazi pamoja na Mbunge wa jimbo la Ulyankulu wilaya ya Kaliua John Peter Kadutu alipotembelea taasisi hiyo.

Amesema wakazi wa vijiji vinavyozunguka pori hilo la akiba wamekuwa wakifanya shughuli za kilimo ndani ya mto Igombe hali inayohatarisha uwepo wake.

Afisa huyo ametaja vitendo vingine vinavyohatarisha mto huo ni wafugaji kulishia mifugo yao ndani ya mto huo na ndani ya hifadhi licha ya sheria kukataza vitendo hivyo.

Thomas ametoa mfano wa  mkazi mmoja wa kijiji kimojawapo kinachopakana na pori hilo la akiba alithubutu kujenga ndani ya mto huo.

Afisa huyo amelalamikia viongozi wa serikali za vijiji hivyo vya jirani kutotoa ushirikiano  kwa maofisa hao wahifadhi katika kuwabaini na kuwachukulia hatua waharibifu hao hali inayosababisha ugumu katika kukabiliana na vitendo hivyo.

Amesema mto huo ni muhimu sana  kwa maisha ya wanyama na viumbe hai waliopo katika pori hilo la akiba na kwamba ukitoweka utaharisha maisha ya viumbe hao. 

Akizungumzia suala hilo mbunge wa Ulyankulu John Peter Kadutu amesema ni wajibu wa viongozi wa serikali za vijiji vinavyozunguka pori hilo kuheshimu sheria na kuacha tabia ya kushirikiana na watu wanaovunja sheria kwa kufanya shughuli za kilimo, uvuvi, uwindaji, upasuaji mbao au kuchoma moto maeneo ya hifadhi.

Amesema viongozi hao wa vijiji wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kuacha kupokea rushwa au hongo kutoka kwa watu wanaovamia hifadhi hiyo kwa lengo la kulima au kuchungia mifugo.

Hata hivyo Kadutu amewataka maofisa hao uhifadhi wa pori la akiba la Kigosi Moyowosi kanda ya Kusini kutoa elimu kwa jamii kuhusu uhifadhi na pia kusaidia shughuli za kijamii katika maeneo yao hali itakayosaidia kukuza ushirikiano katika kulinda na kuendeleza pori hilo la akiba.

No comments: