Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Friday, January 8, 2016

ASKARI WA ULYANKULU WALALAMIKIWA KUWATOZA WANANCHI FEDHA ZA MAFUTA



Mh. Mbunge John  Peter Kadutu akizungumza na askari wa kituo cha Ulyankulu

 
Na Paul Christian,Ulyankulu

Askari polisi wa kituo cha Ulyankulu wilaya ya Kaliua mkoani Tabora wamelalamikiwa kudai malipo ya shilingi 300,000/= kutoka kwa wananchi kama gharama ya mafuta ya kuwafikisha kwenye matukio ya kihalifu.

Akizungumza na askari hao mbunge wa jimbo la Ulyankulu John Peter Kadutu amesema hivi karibuni askari hao walidai wapewe kiasi hicho cha fedha ili waweze kufika kijiji cha Sasu kulipotokea uhalifu.

Amesema kitendo cha kudai fedha kutoka kwa wananchi ili watekeleze majukumu yao ni miongoni mwa kero walizonazo wananchi wa jimbo hilo dhidi ya askari hao.

Kadutu amewataka askari hao kuacha kuwaomba fedha wananchi kwa kuwa ni ukiukaji wa sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza shughuli za utekelezaji wa majukumu yao.

Mbunge huyo ameweka bayana kuwa endapo askari hao watatenda haki kwa kuacha kuwaonea wananchi kwa kuwaomba fedha za mafuta, kupokea rushwa na kuwabambika kesi hawataingiliwa katika kutimiza majukumu yao.

Kadutu amebainisha kuwa kila mkazi wa jimbo hilo angependa kuishi kwa amani na utulivu huku akijikita zaidi kwenye shughuli za uzalishaji mali badala ya kuhangaikia kesi za kutengenezwa na askari hao kwa lengo  la kujipatia fedha isivyohalali.

Amesema, “kumekuwa na malalamiko mengi juu yenu jambo ambalo linapaswa kuangaliwa kwa kutekeleza majukumu yenu kwa mujibu wa taratibu zenu badala ya kutanguliza tamaa ya kujinufaisha.”

Mbunge huyo wa Ulyankulu amewahimiza askari hao kuacha vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu kwa kuwapiga watuhumiwa au kuwanyanyasa kwa namna yoyote hata kama wametii kuwa chini ya ulinzi.

Kadutu amebainisha kuwa vitendo hivyo vinazidi kuchochea chuki kutoka kwa wananchi hali ambayo inadhoofisha dhana nzima ya polisi jamii, ulinzi shirikishi na utii wa sheria pasipo shuruti.

Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kaliua Haruna Kasele amekemea tabia ya baadhi ya askari hao kuvujisha siri wanazopewa na raia wema kuhusu uhalifu au wahusika wa uhalifu kwa nia ya kujinufaisha.

Amesema tabia hiyo ni kinyume na maadili ya jeshi la polisi na imewafanya wananchi kujitojihusisha na jeshi hilo katika kusaidia kupambana na uhalifu katika jimbo hilo la Ulyankulu.

Mbunge wa Ulyankulu John Peter Kadutu amefanya ziara ya siku ya tatu ya kutembelea taasisi za umma na binafsi kwa lengo la kupokea ushauri, kero na maoni kabla ya kuanza vikao vya bunge Januari 26 mwaka huu.

No comments: