Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, January 17, 2016

HALMASHAURI YA WILAYA YA KALIUA YALALAMIKIWA NA WATUMISHI WA AFYA

BAADHI YA WATUMISHI WA KITUO CHA AFYA ULYANKULU WILAYA YA KALIUA MKOANI TABORA


Na Paul Christian, Ulyankulu.

Halmashauri ya wilaya ya Kaliua mkoani Tabora imelalamikiwa kutowalipa malipo ya kazi za ziada watumishi wa kituo cha afya Ulyankulu wanapoambatana na wagonjwa wa rufaa kuwapeleka hospitali ya wilaya ya Urambo au kwingineko.

Watumishi hao wametoa malalamiko hayo hivi karibuni kufuatia mbunge wa jimbo la Ulyankulu John Peter Kadutu kufanya ziara ya kikazi katika kituo hicho kinachohudumia wakazi wa kata 18 za tarafa ya Ulyankulu wilayani humo.

Wamesema walipokuwa chini ya halmashauri ya wilaya ya Urambo walikuwa wakilipwa malipo ya kazi za ziada jambo ambalo halifanyiki katika halmashauri ya wilaya ya Kaliua.

Afisa muuguzi Fatuma Shaban amebainisha kuwa kutokana na kituo hicho kukabiliwa na upungufu wa watumishi wanalazimika kufanya kazi hadi saa za ziada lakini wanapoomba kulipwa fedha za muda huo wamekuwa wakilipwa kidogo na yanachukua muda mrefu.

Naye dereva wa gari la wagonjwa Adrey Mkini ameitaka halmashauri hiyo iwe inamlipa madai yake ya kazi za ziada ndani ya muda mfupi baada ya kuwasilisha madai yake ili aweze kupata fedha za kulihudumia gari hilo.

Amesema, “Gari linapopata pancha au matatizo mengine madogo madogo ni malipo hayo ya kazi za ziada nayatumia kulihudumia.”

Aidha muuguzi Shida Juma Katindili ameitaka halmashauri hiyo kuwapatia sare angalau mara mbili kwa mwaka kwa kuwa wanapata shida kuvaa sare moja kwa mwaka mzima.

Mtaalamu wa maabara Josia Raphael Bitulo ameitaka idara ya afya kuwatimizia mahitaji ya vifaa tiba vya maabara kulingana na maombi yao ili waweze kutoa huduma yenye tija kwa wagonjwa.

Mlinzi wa kituo hicho Simon Kamugwa amesema amekuwa akifanya kazi ya ulinzi peke yake tangu mwaka 2012 baada ya mwenzake kustaafu hali inayomsababisha kufanya kazi hata wakati akiwa anaumwa.

Mlinzi huyo ameitaka halmashauri hiyo kuongeza walinzi kwa kuwa kituo hicho ni kikubwa na kina mali nyingi ikiwemo gari la wagonjwa.

Akijibu madai hayo ya watumishi, mwenyekiti wa kamati ya huduma ya afya, Elimu na Maji kwenye halmashauri ya wilaya ya Kaliua Alphonce Msanzya amesema madai yote wameyachukua na wanakwenda kuyafanyia kazi.

No comments: