Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, January 13, 2016

WAKAZI WA TARAFA YA ULYANKULU WANATESEKA KWA UKOSEFU WA BENKI NA VITUO VYA MAFUTA


MBUNGE WA ULYANKULU JOHN PETER KADUTU AKIZUNGUMZA NA WAFANYABIASHARA, WENYEVITI WA  VITONGOJI NA VIJIJI JIMBONI HUMO


Na Paul Christian, Ulyankulu.

Wakazi  wa tarafa ya Ulyankulu wilaya ya Kaliua mkoani Tabora wamesema wanateseka kwa kukosa huduma za kibenki pamoja na vituo vya mafuta hali inayowafanya wasafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo.

Kero hizo ziliainishwa na watumishi wa umma,wafanyabiashara,vyama vya masingi vya ushirika na viongozi wa dini wakati  wakizungumza kwa nyakati tofauti na mbunge wa jimbo la Ulyankulu wilayani humo John Peter Kadutu alipofanya ziara ya kikazi jimboni humo.

Wamesema ukosefu wa huduma za kibenki katika tarafa hiyo unawasababisha kusafiri umbali wa kilometa 90 au zaidi kufuata huduma hizo wilaya ya Urambo au Tabora mjini na hivyo kuwagharimu fedha nyingi na muda mwingi ambao ungetumika kuzalisha mali.

Wakazi hao wamesema hali hiyo imewafanya wafanyabiashara na wafanyakazi kutembea na fedha nyingi mkononi hali inayohatarisha maisha na mali zao kwa kuwa matukio ya uhalifu yamekuwa yakiwalenga mara kwa mara.

Wakizungumzia ukosefu wa vituo rasmi vya kuuza mafuta ya petroli,dizeli ,mafuta ya taa pamoja na bidhaa nyingine za vyombo vya moto  wamesema  taasisi za umma na binafsi zimekuwa zikipata usumbufu kutimiza masharti ya sheria ya manunuzi kwa kuwa huduma hizo zinapatikana zaidi ya kilometa 90 kutoka tarafa hiyo.

Aidha wakazi hao wamebainisha kuwa kero hizo ni miongoni mwa sababu zinazowafanya watumishi wa umma kushindwa kukaa kwa muda mrefu kufanya kazi  tarafani humo.

Akijibu hoja hizo mbunge  wa jimbo hilo John Peter Kadutu amewaambia wakazi hao kuwa suala la benki linashughulikuwa kwa kuwa tayari Milambo SACCOS  iliyopo barabara ya 13 tarafani humo inalo jengo lenye miundombinu ya kibenki na kinachohitajika ni mwekezaji tu.

Mbunge huyo amesema analifuatilia suala hilo jijini Dar es Salaam ambapo atazungumza na mkurugenzi wa benki ya CRDB ambayo ni mdau mkubwa wa SACCOS hiyo kwa kusaidia ramani ya jengo na mambo mengine.

Kuhusu vituo vya mafuta Kadutu amesema atalifikisha suala hilo kwa makampuni yanayofanya biashara hiyo ili kuona uwezekano wa  kuwekeza kwenye tarafa ya Ulyankulu.

Hata hivyo mbunge huyo amewatia moyo watumishi wa umma wanaofanya kazi katika tarafa hiyo kwamba kero zilizopo sasa zimeanza kushughulikiwa na zitatatuliwa moja baada ya nyingine.

No comments: