Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, December 20, 2015

WAKULIMA :WALALAMIKIA UCHELEWESHAJI WA PEMBEJEO ZA RUZUKU.



Na Nicholaus Kagusa, Tabora.

Wakulima wa kijiji na kata ya Malolo katika Manispaa ya Tabora wamesema ucheleweshwaji wa pembejeo za ruzuku umesababisha wakulima wasio na uwezo kushindwa kufikia  malengo ya kilimo chenye tija.

Mkulima wa kijiji hicho Khadija Mdemi amesema pembejeo hizo zimechelewa kufika ambapo mbegu na mbolea za kupandia zimefika wakati mimea ya mahindi imekwisha ota.

Mkulima huyo amebainisha kuwa vocha za pembejeo hizo zinawafikia wakulima wachache ukilinganisha na idadi ya kaya masikini zinazohitaji kujikwamua kupitia kilimo.

Naye Tilizo Kasto mkulima wa kijiji cha Malolo amesema kuwa mara kadhaa mbegu za kisasa zinazotolewa kwenye mpango huo zimekuwa hazioti jambo lililomgharimu kutafuta mbegu za mahindi aina nyingine.

Mkulima huyo pia ameeleza kuwa mara nyingi mifuko ya mbolea pamoja na mbegu inawafikia ikiwa na ujazo pungufu kutokana na hujuma. 

Akizungumzia hali hiyo mwenyekiti wa kamati ya Vocha yenye wajumbe sita katika kijiji hicho Rehema Lukaya amesema upungufu wa mbolea na mbegu za ruzuku zinazotolewa kwa wakulima hao unatokana na baadhi yao kuziuza kwa watu wenye uwezo na hivyo kupoteza maana halisi ya mpango huo.

Afisa mtendaji wa kijiji hicho ambaye pia ni afisa pembejeo wa kata ya Malolo Paulo Thobias Suwi amesema wakala aliyepewa kandarasi ya kusambaza pembejeo hizo  ni John Mchele Enterprises na kwamba alianza kufikisha pembejeo hizo mnamo Novemba 27 mwaka huu.

Kutokana na kauli hiyo ya Afisa mtendaji ni dhahiri kuwa Novemba 27 ni muda ambao wakulima wengi walikuwa wamepanda mahindi katika mashamba yao hivyo mbegu na mbolea za kupandania zilichelewa kuwafikia wakulima hao.

Aidha Paulo alifafanua kuwa wakala huyo kabla ya kukabidhi pembejeo huwa anaipima mifuko ya mbolea na mbegu ili kuhakikisha ujazo wake tofauti na ilivyokuwa huko nyuma.

Meneja wa kampuni ya John Mchele Enterprises Juma Abdallah amesema wamepewa kandarasi ya kusambaza pembejeo hizo katika kata tatu za Malolo, Itetemia na Kabila na wamekuwa wakijitahidi kuwahisha pembejeo kwa wakulima.

Amesema kampuni yake pia inalojukumu la kuhakikisha ujazo wa mbolea na mbegu uko sawa kulingana na maelezo ya mkataba kabla ya kuwakabidhi wakulima.

Afisa Kilimo wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Ditirick Mwinuka amesema mpango wa pembejeo za ruzuku unaotoa mbolea za Minjingu, UREA, DAP, CAN pamoja na mbegu za mahindi aina chotara na kwamba unahudumia  vijiji 11 katika manispaa hiyo.

Amesema Halmashauri hiyo ilifanya makadirio ya vocha 5,000 lakini ikapokea vocha 1,312 sawa na kaya 11,000.

Mwinuka amebainisha kuwa mpango huo unagusa kaya masikini ambazo hujengewa uwezo kwa kupewa pembejeo hizo kwa muda wa miaka mitatu mfululizo kabla ya mpango huo kuhamia kwa kaya nyingine masikini.




No comments: