Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, December 9, 2015

KESI NDOGO YA KUOMBA KUPUNGUZIWA DHAMANA KUAMULIWA DISEMA 14 MWAKA HUU.

Na, Murugwa Thomas, Tabora


MAHAKAMA  KUU kanda ya Tabora imesikiliza kesi ndogo ya kuomba kutokulipa ama kupunguziwa dhamama ya gharama ya kesi ya kupinga matokeo ya ubunge jimbo la Tabora mjini na kwamba itatoa uamuzi  Disemba 14 mwaka huu.


Hatua hiyo imefikiwa na jaji mfawidhi wa Mahakama ya Kuu kanda ya Tabora Amir Mruma baada ya kusikiliza maombi ya wanachama wanne wa Chama Cha Wananchi CUF waliofungua shauri hilo pamoja na pingamizi la walalamikiwa.



Wanachama hao wakiwakilishwa na wakili msomi wa kujitegemea Hashim Mziray  katika maombi yao wanaiomba mahakama iwakadirie kiwango waanachoweza kulipa kama dhamana ya kesi ama iwasamehe wasilipe chochote  katika shauri lao namba 3/2015 la kupinga matokeo ya uchaguzi.



Pia wameiomba Mahakama Kuu iwarejeshee gharama zao kwa namna itakavyona kwa kuwa wanakipato kidogo  ambacho kinawasaidia kumudu maisha ya familia zao kwani wao ni wajasiriamali wadogo na wanawategemezi..



Aidha maombi hayo yalipingwa na mawakili Kamaliza Kayaga anayemwakilisha mlalamikiwa wa kwanza Emanuel Mwakasaka na wakili mwandamizi wa serikali Juma Masanja anayewawakilisha  walalamikiwa wawili kwa madai kwamba hawakuleta ushahidi wa uthibitisho kwenye maombi yao ya kiapo.



Mawakili hao walidai kuwa endapo walalamikaji wasingekuwa na uwezo wangeenda kwenye mashirika ya msaada wa kisheria kuomba msaada lakini wao wameweza kumkodi wakili msomi kutoka jiji Dar es salaam hivyo wanao uwezo mkubwa wa kifedha.



Waliongeza kuwa mahakama hiyo inabidi itilie maanani kuwa endapo walalamikaji watashindwa kesi ya msingi watashindwa kuwalipa walalamikiwa gharama za uendeshaji wake ambazo wameisha anza kuingia katika shauri hilo.



Kutokana na hali hiyo wameiomba mahakama iwape nafasi kwa kuzingatia matakwa ya sheria ya kesi za uchaguzi walipe walau kiasi cha fedha kama dhamana ili kuwe na ulinganifu kama ambavyo imefanya katika maamuzi yake kwenye kesi za aina hiyo zilikwisha funguliwa mwaka huu.



Wananchama wanne wa Chama Cha Wananchi CUF wamefungua kesi mahakama kuu kupinga matokeo ya uchaguzi wa jimbo la Tabora mjini ambalo Emanuel Mwakasaka wa CCM alishinda kwa  kura  44,114 dhidi ya kura 35,452  alizopata Peter Mkufya  wa CUF akiungwa mkono na vyama vyanavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi, UKAWA.



Wanachama hao Jumanne Mtunda, Johari Kasanga, Thomas Omoth na Shaban Mussa wamefungua kesi hiyo  Na. 3/2015 wakidai  mahakama iwape haki yao ya msingi kama wapiga kura kwa kuwarejeshea mbunge waliomchagua  Peter  Mkufya.

MWISHO.

No comments: