Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Monday, December 7, 2015

Dr. MAGUFULI MFUMO DHAIFU WA SEKTA YA AFYA UNADHOOFISHA NGUVU KAZI YA TAIFA

Na Paul Christian, Tabora.


Mwanasayansi Muingereza Sir Isaac Newton aliyezaliwa Januari 4,1643 na kufa Machi,31,1727 aliwahi kusema, “I can calculate the motion of heavenly bodies, but not the madness of people.”

Kwa lugha ya Kiswahili mwanasayansi huyo alimaanisha, kwake ilikuwa rahisi kufanya hesabu ya  mwendo wa vitu mbalimbali, lakini kamwe asingeweza kufanya hesabu kujua kiwango cha uwendawazimu kwa watu.


Sir Isaac Newton,ananikumbusha kuitazama serikali ya Tanzania na mkakati wake wa makusudi wa kujenga msingi wa watu wake kuwa na Afya  Bora  kutokana na chakula, matunda pamoja na vinywaji wanavyokunywa.

Tanzania imekuwa dampo la utamaduni, vyakula na vinywaji  kutoka ndani na nje ambavyo havina ubora wala umuhimu kwa afya, huku serikali ikichukua hatua hafifu kulinda afya za watu wake kwa kuzuia uingizaji na utengenezaji holela wa vitu hivyo.

Kama Taifa nilitegemea kuona mkakati wa vitendo usiotiliwa shaka kwa serikali kuwajenga watu wake toka utotoni hadi uzeeni kwa kuwa na tabia ya kuzingatia lishe bora kama msingi imara wa kuondokana na magonjwa yakitabia.

Uwendawazi anaouzungumza mwanasayansi Sir Isaac Newton ulionekana mwaka 2011 ilipozuka dawa ya muujiza maarufu kama “kikombe cha babu” iliyotolewa kwa hisani ya Mchungaji mstaafu wa KKKT, Ambilikile Mwasupile katika kijiji cha Samunge wilaya ya Loliondo.

Dawa  hiyo ya kimuujiza ilidaiwa kutibu magonjwa yote ikiwemo magonjwa sugu ya Kisukari na UKIMWI, mamia kwa maelfu ya watanzania wakamiminika kwa babu ili waweze kupata kikombe cha dawa kwa Tshs. 500 tu.

Maajabu hayo yalikuzwa na vyombo vya habari na kuungwa mkono na serikali ya Dr. Jakaya Mrisho Kikwete kwa mawaziri wake akiwemo Rais wa sasa Dr. John Pombe Magufuli kukimbilia Samunge kupata muujiza.

Jambo muhimu  hapa ni kwamba dawa hiyo ya “Babu” inatokana na mmea ambao kwa wamaasai unajulikana kama Engamuriaki” au “Olmuriaki na kwa Wasonjo unajulikana Engamuriaga.” 

Aidha Kitaalamu mmea huo unajulikana  Carissa spinarum” ( Carissa edulis) ambao ni miongoni mwa mimea familia ya “Apocynaceae” na unapatikana katika nchi nyingi ikiwemo Kenya, Uganda, Sudan Kusini,Sudan, Ethiopia, Cameroon, Eritrea, Senegal, Ghana, Nigeria na Botswana.

Pia unapatikana katika nchi za Afrika Kusini, Namibia, Guinea, Australia, Cambodia, Japan, Myanmar, Namibia, Papua, Saudi Arabia, Thailand,Vietnam na Yemen.

Kwa wamaasai mmea huo “Engamryaki uchanganywa kwenye mziwa au  supu ya nyama, na  mizizi yake imekuwa ikiwekwa kwenye vibuyu vya kuhifadhia maji ili kuyapa ladha inayovutia.

Jamii nyingine za wafugaji nchini Tanzania kwa maana ya wasonjo, wagogo, wakurya na wabarbaig zimekuwa zikiutumia mmea huo kama dawa.

Nchini Ghana matunda ya mmea huo ambayo ni mazuri na matamu yamekuwa yakitumika kama kiungo cha kuchochea hamu ya kula kwa wagonjwa, na katika nchi za Kenya na Sudan umekuwa ukitumika kutengenezea   jam.

Mmea huu wa Carissa edulis” unatumika kutibu magonjwa mbalimbali kama vile kifafa,maumivu ya kichwa, maumivu ya kifua, Kisonono, Kaswende,Kichaa cha mbwa,selimundo, upungufu wa damu,homa na ngiri.

Magonjwa mengine yanayoweza kutibiwa na mmea huo ni Kisukari,Presha,kurekebisha mfumo wa Ini,saratani na magonjwa mengine sugu.

Kimsingi mmea huu  umetumika kama tiba miaka elfu iliyopita ambapo katika nchi ya India na maeneo ya jirani umekuwa ukitibu kuharisha na magonjwa mengine.

Uwendawazimu usioweza kufanyiwa mahesabu na Sir Isaac Newton niliuona pale serikali ya Tanzania ilipokaa kimya kuona mamia kwa maelfu ya wananchi wake wakiacha kutumia dawa za kisayansi baada ya kunywa kikombe cha babu. 

Tafsiri ya mamia kwa maelfu ya watanzania kufurika kwa babu kupata tiba ya Kikombe inamaana kuwa Tanzania inawananchi wengi wenye afya dhaifu kwa magonjwa  yasiyokuwa na uhakika wa tiba.

Kikombe cha Babu wa Samunge kuliiumbua serikali ya Tanzania kwa kuionyesha kuwa inasimamia mfumo dhaifu wa afya na ndio maana watu wake wengi wanahitaji muujiza wa uponyaji kwa gharama yoyote.

Kwa nini serikali ya Tanzania ilishabikia na kuunga mkono uvumi wa miujiza ya uponyaji kupitia dawa ya Kikombe cha Babu badala ya kufanya utafiti wa kutosha kujiridhisha na hali halisi ya kile kilichodaiwa ni muujiza wa uponyaji.

Swali la kujiuliza hapa ilikuwaje mmea huo unaojulikana kwa karne kadhaa  kama dawa ya kutibu magonjwa mbalimbali ukapewa sura mpya ya kuwa na maajabu ya kipekee kupitia Kikombe cha Babu wa Samunge?

Na kama ni kweli mmea huo ulikuwa na upako na nguvu ya kipekee katika kutibu magonjwa sugu kama Kisukari, Saratani na UKIMWI, upako na uwezo huo wa kiuponyaji umeenda wapi kwa sasa?

Serikali ya Tanzania ilijifunza nini kwa kuwa na viongozi wenye afya dhaifu kama ilivyokuwa kwa wananchi wake ambao mamia kwa maelfu walimiminika kwa babu ili kupata kikombe kuponya magonjwa yao ambayo yameshindikana kutibiwa mahali pengine?

Tafsiri nyingine ni kwamba taifa halina mipango, vipaumbele au mkakati wa makusudi wa kuimarisha afya za watu wake kupitia lishe bora pamoja na  huduma bora za afya ndio maana linategemea miujiza  kama ile ya “Kikombe cha Babu.”

Watanzania wengi wanasumbuliwa na magonjwa yatokanayo na tabia ya kula vyakula na kunywa vitu visivyokuwa na manufaa kwa miili yao na hii inatokana na udhaifu wa mfumo wa umma katika kutoa elimu sahihi kuhusu lishe bora.

Licha ya uwepo wa mamlaka zinazosimamia mambo ya lishe, kama taifa hakuna mkakati wa namna gani serikali inataka watu wake wawe na utaratibu sahihi katika ulaji na unywaji wao ili kujenga taifa la watu wenye afya madhubuti.

Uduni wa Lishe kwa watanzania unaonekana kwa watu wa matabaka yote, wasomi, wasio wasomi, wamijini na wavijijini.

Miujiza ya “Kikombe cha Babu” hata sasa bado inaendelea kwa kuibuka wimbi la watu wanaojiita wataalamu wa tiba mbadala  ambao wengi wao wanautumia mwanya wa serikali ya Tanzania kutojishughulisha na afya za watu wake.

Na kwa kuwa hiyo ndio hali halisi ujenzi wa uchumi wa kati na Tanzania yenye viwanda unategemea kujengwa na watu wenye afya za namna gani?

*****************************













No comments: