Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Tuesday, December 15, 2015

ALMASI MAIGE: AKANUSHA UVUMI WA KUSIMAMISHWA BUNGENI PAMOJA NA KUHUSIKA NA UTOROSHAJI MAKONTENA BILA KULIPA USHURU.



Na Paul Christian,Tabora.

Mbunge wa Jimbo la Tabora Kaskazini, wilaya ya Uyui mkoani Tabora Mheshimiwa Almasi Maige amekanusha uvumi unaoenezwa na watu wasiojulikana kwamba amesimamishwa kujihusisha na shughuli za Bunge kwa muda wa miezi sita kwa madai ya kuvunja kanuni kwa kuongea na simu ya mkononi akiwa ndani ya moja ya vikao vya Bunge hilo mjini Dodoma.

Akiongea kwa njia ya simu na mwandishi wa Voice Of Tabora FM leo asubuhi mbunge huyo amesema hajawahi kusimamishwa na Spika wa Bunge hilo kwa kinachodaiwa kuvunja kanuni kwa kuongea na simu ya mkononi akiwa ndani ya ukumbi wa bunge wakati wa mkutano wa kwanza wa Bunge la 10.

Mheshimiwa Maige amefafanua kuwa katika mkutano huo wa kwanza hakuna mbunge hata mmoja aliyesimamishwa kwa madai ya kuvunja kanani za Bunge kwa kuongea na simu wakati vikao vikiendelea.

Mbunge huyo wa Jimbo la Tabora Kaskazini amesema, “mimi sio mgeni wa kanuni za Bunge kwa kuwa nimekuwa mbunge wa Bunge la Katiba la mwaka 2014, hivyo nafahamu na kuzielewa kanuni vizuri.”

Aidha Mheshimiwa Maige amekanusha uvumi kuhusika na biashara ya utoroshaji wa makontena  kutoka bandari ya Dar es Salaam na kukwepa kulipa ushuru kwa kuwa yeye si mfanyabiashara wa makontena.

Amesema, “mimi si mfanyabiashara wa makontena, biashara yangu ni ya mawasiliano na ulinzi wa kisasa wa kufunga mitambo.”

Mheshimiwa Maige amewataka wananchi wa Jimbo la Tabora Kaskazini kuwapuuza watu hao wanaovumisha mambo yasiyofaa kwa malengo wanayoyajua wao ambayo hayana maslahi kwa wananchi wa jimbo hilo.

Amebainisha kuwa uvumi huo unatungwa na kusambazwa na watu wasiokuwa na busara na kwamba watu hao wanapaswa kutambua uchaguzi umekwisha na sasa ni wakati wa kuchapa kazi.

Mheshimiwa Maige amebainisha kuwa kwa sasa yuko jijini Dar es Salaam akiendelea na zoezi la utafiti kuhusu matatizo yanayolikabili zao la tumbaku na kutafuta ufumbuzi wa matatizo hayo, zoezi ambalo amelianza mara baada ya kuahirishwa kwa mkutano wa kwanza wa Bunge la 10.

Amesema katika utafiti wake wa awali alifanya ziara ya kutembelea wadau wa zao la Tumbaku mkoani Tabora ambao ni makampuni yanayonunua tumbaku, Bodi ya Tumbaku TTB, mlajisi wa vyama vya Ushirika pamoja na taasisi za fedha.

Mheshimiwa Maige ameeleza kuwa akiwa jijini Dar es Salaam anaendelea na utafiti huo ambao utasaidia kukabiliana na changamoto za kilimo cha tumbaku ambacho kimekuwa kikilalamikiwa kwa kukosa tija na wakulima wa zao hilo jimbo la Tabora Kaskazini.

Amesema, “hauwezi kuongelea Tabora bila ya Tumbaku, bila ya wadau wa Tumbaku.”

Mkutano wa kwanza wa Bunge la 10 ulianza tarehe 13 hadi 20 Novemba, 2015 ambao ulikuwa na shughuli mbalimbali ikiwemo kuchaguliwa kwa Spika wa Bunge  na baadaye kuapishwa, kuapishwa kwa wabunge, kuthibitisha uteuzi wa waziri mkuu, kuchaguliwa kwa Naibu Spika na hatimaye Rais Magufuli kulihutubia na kulizindua Bunge.

No comments: