Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Monday, December 14, 2015

MWALIMU ADAIWA KUTOWEKA NA ZAIDI YA TSH. MIL. 2.8 ZA WANAFUNZI



Na Lucas Raphael,Igunga.

Mwalimu mmoja anayefundisha shule ya Sekondari Igunga Day iliyopo wilayani Igunga mkoa wa Tabora anatuhumiwa kutoroka na fedha za wanafunzi wa shule hiyo zilizochangwa kwa ajili ya kuwawezesha kufanya ziara ya masomo katika hifadhi ya Ngorongoro.

Mwalimu huyo Paulo Msabila anadaiwa kuwachangisha wanafunzi hao Tshs. 50,000/= kila mmoja kwa lengo la kutembelea hifadhi hiyo yenye umaarufu wa kipekee Duniani.

Akizungumzia tukio hilo mmoja wa wazazi wa wanafunzi hao Rashid Mgendi alisema alitoa Tshs 50,000/= kwa ajili ya mtoto wake Juma Rashid anayesoma kidato cha pili katika shule hiyo ili aweze kushiriki ziara hiyo ya mafunzo iliyoyeyuka bila maelezo.

Joseph Nyangi ni mzazi wa mwanafunzi Bahati Marwa anayesoma kidato cha tatu ambaye alitoa kiasi cha Tsh 50,000/= kwa ajili ya kumuwezesha mtoto wake kwenda kujifunza katika hifadhi hiyo ya Ngorongoro alishangazwa na kitendo cha mwalimu huyo kutoweka na fedha zao.

Wazazi hao walisema kuwa baada ya kuona ziara hiyo ya mafunzo imeshindikana walikwenda kumuona mwalimu huyo ili arejeshe fedha walizochanga lakini mwalimu huyo hakufanya hivyo hadi shule hiyo imefungwa kwa  likizo.

Aidha mwalimu huyo hajulikani alipo na hata simu yake ya mkononi haipatikani licha ya kutafutwa kwa zaidi ya wiki moja.

Mkuu wa shule hiyo ya sekondari Igunga day ,Nelson Edward alikiri kuwa mwalimu huyo  aliwachangisha wanafunzi wa shule hiyo zaidi ya shilingi milioni 2.8 ambazo hakuzitumia kwa lengo lililokusudiwa na badala yake alizitumia kujinufaisha.

Kaimu afisa elimu sekondari wilayani Igunga Fred Matalu amekiri kutokea kwa tukio hilo na kwamba ameitaka bodi ya shule hiyo kuchukua hatua.

No comments: