Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, December 20, 2015

HALMASHAURI YA WILAYA YA KALIUA KUFIKISHWA MAHAKAMANI



Na Halima Ikunji, Tabora.

Kampuni ya Ujenzi ya SARAM ya jijini Dar es Salaam inakusudia kuifikisha mahakamani halmashauri ya wilaya ya Kaliua mkoani Tabora kwa kuvunja mkataba wa ujenzi bila makubaliano ya pande mbili.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Tabora meneja wa kampuni hiyo Raymond Mkandawile amesema aliingia mkataba na halmashauri hiyo ya kujenga nyumba nne za watumishi, jengo la wagonjwa wa nje la hospitali ya wilaya OPD,ofisi ya mkurugenzi pamoja na jengo la maonesho ya nane nane katika mtaa wa Ipuli mjini Tabora.

Meneja huyo amesema mkataba wa kujenga majengo hayo umevunjwa na halmashauri hiyo huku wakiwa wanaidai jumla ya shilingi milioni 234.
Mkandawile alifafanua kuwa katika ujenzi wa OPD wanadai Tsh. Mil.110, nyumba nne za watumishi Tsh. Mil. 54 na jengo la ofisi ya mkurugenzi  Tsh. Mil 70.

Alisema, “tumesikitishwa sana na uamuzi wa kikao cha madiwani wa halmashauri hiyo kilichokaa mwezi huu na mkurugenzi wa halmashauri hiyo Athumani Kihami kutangaza kuvunja mkataba na kampuni yetu kwa madai tumekiuka mkataba jambo ambalo si kweli.”

Mkandawile ameeleza kuwa kitendo hicho cha halmashauri ni udhalilishaji wa kampuni ya SARAM ambayo imejenga majengo hayo kwa asilimia 99, isipokuwa halmashauri hiyo iliingia kwenye nyumba hizo nne pasipo makabidhiano ya aina yoyote.

Aidha amesema kuwa kilichotokea katika maeneo ya ujenzi walisimamisha  ujenzi kutokana na halmashauri hiyo kuchelewesha malipo hali iliyosababisha wafanyakazi wa kampuni hiyo kushindwa kulipwa stahiki zao kwa wakati.

Meneja huyo alikanusha madai kuwa kampuni yake iliitwa mara kadhaa kwenye vikao vya mazungumzo kujadili kuhusu mkataba wa huo na haikutuma mwakilishi.

“Hatujawahi kupokea barua yoyote ya wito kutoka katika halmashauri hiyo kwa lengo la mazungumzo.”Amesema meneja huyo.

Awali mwenyekiti wa halmashauri hiyo Haruna Kasele alisema kampuni hiyo iliitwa zaidi ya mara tatu katika meza ya mazungumzo lakini haikutokea, ndipo baraza la madiwani likaridhia kuvunjwa kwa mkataba huo.

Kwa upande wake  mbunge wa jimbo la Kaliua Magdalena Sakaya amemtaka mkurugenzi wa halmashauri hiyo kuwapa madiwani mkataba huo uliovunjwa ili waupitie na kubaini kiini cha mgogoro huo.

Amemtaka mkurugenzi  huyo kutotangaza upya tenda ya ujenzi wa majengo hayo hadi pale madiwani watakapojiridhisha baada ya kuupitia mkataba huo.

No comments: