Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, December 9, 2015

Katika Historia:MAKOMANDOO WA ISRAEL WALIVYOWAOKOA MATEKA WA NDEGE YA SABENA.









Tarehe 8 Mei 1972, ndege hiyo aina ya Boeing 707 -329 ikiongozwa na rubani muingereza Reginald Levy ilitekwa nyara na watekaji wanne kutoka kundi lililojulikana “Black September.”

Utekaji huo ulipangwa na Ali Hassan Salameh na kuwahusicha watekaji wanne wawili wanaume na wawili wanawake wakiwa na silaha aina ya bastola wakiongozwa na Ali Taha.

Dakika 20 baada ya kuondoka kwenye uwanja wa kimataifa wa Wien-Schwechat jijini Vienna, Austria ,watekaji wakavamia  chumba cha marubani. 

Nahodha wa ndege hiyo Levy alisikika akiwaambia abiria 90 “tumepata marafiki” huku yeye mwenyewe na abiria wakisubiri amri kutoka kwa watekaji hao. 

Jambo moja la kuvutia katika tukio hilo mke wa rubani huyo kiongozi alikuwa miongoni mwa abiria ndani ya ndege hiyo.

Baada ya kuhakikisha wameidhibiti ndege hiyo watekaji waliwatenganisha abiria wenye asili ya Israel na raia wengine, kisha wakawaelekeza waende sehemu ya nyuma ya ndege.

Ndege hiyo ikiwa na abiria 94 wakiwemo watekaji hao wanne ilitua kwenye uwanja wa Lod Airport ambao kwa sasa unajulikana Ben Gurion International Airport jijini Tel Aviv nchini Israel.

 Wakiwa kwenye ardhi ya Israel Watekaji hao walitoa madai yao kwa serikali ya Israel ya kutaka kuachiliwa huru kwa wafungwa 315 wa kipalestina ambao walifungwa nchini humo kwa makosa ya Ugaidi.
 


Katika hali taharuki huku watekaji wakilia na kukumbatiana kama ishara ya kuagana, nahodha wa ndege hiyo Levy aliweza kutuma ujumbe kwa serikali ya Israel akiomba msaada wa kuokolewa.

Waziri wa ulinzi  wa Israel Moshe Dayan akafanya mazunguzo na watekaji hao wakati huo huo  akifanya mipango ya kijeshi ya kuwaokoa mateka hao katika operesheni iliyopewa jina la ISOTOPE.

Tarehe 9 Mei, 1972 majira ya saa kumi jioni operesheni ya kuwaokoa mateka ikaanza ambapo timu ya makomandoo 16 wa kikosi cha Sayeret Matkal wakiongozwa na Ehud Barak na Benjamini Netanyahu waliikaribia ndege hiyo iliyotekwa.

Viongozi hao wa operesheni ISOTOPE  baadae walishika wadhifa wa uwaziri mkuu wa Israel ambapo Benjamini Netanyahu ndio waziri mkuu wa sasa wa nchi hiyo.

Makomandoo hao wakiwa wamevalia maovaroli ya rangi nyeupe walijifanya mafundi wa ndege na kuwashawishi watekaji waamini kuwa ndege hiyo ilihitaji matengenezo.

Makomandoo hao wakaivamia hiyo ndege na kuidhibiti ndani ya dakika 10 ambapo waliwaua watekaji wawili wanaume na kuwaweka chini ya ulinzi watekaji wawili wanawake.

Abiria wote waliokolewa, watatu kati yao walijeruhiwa ambapo mmoja wa majeruhi hao baadae alipoteza maisha, Benjamini Netanyahu alipigwa risasi begani katika operesheni hiyo.

Wale mateka wawili wanawake walihukumia kifungo cha maisha jela lakini baadae waliachiwa huru katika mpango wa kubadilishana wafungwa  baada ya vita ya Lebanon ya mwaka 1982.

Ndege hiyo iliyotekwa iliendelea kufanya kazi kwa miaka mitano chini ya shirika la SABENA kabla ya kununuliwa na jeshi la Israel, ambapo ilibadilishwa matumizi na kuwa ndege ya kipelelezi kwa miaka mingi.

Nahodha wa ndege hiyo  Reginald Levy alikuwa ni askari wa kikosi cha anga cha Uingereza ambapo alishiriki kuishambulia Ujerumani katika vita ya pili ya Dunia na alijiunga na shirika la ndege la Ubelgiji SABENA mwaka 1952.

Alistaafu kazi ya urubani mwaka 1982 na akiwa nyumbani kwake Dover alifariki kwa ugonjwa wa saratani tarehe 1 Agosti, mwaka 2010. 

Wakati wa tukio la kutekwa kwa ndege aliyokuwa akiingoza alikuwa akisheherekea siku yake ya kuzaliwa ya mara ya hamsini.

                                                    0684 329 990,paulkagenzi@yahoo.com

No comments: