Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Monday, December 28, 2015

WAFANYABIASHARA WACHANGIA UKARABATI KITUO CHA POLISI



Na Elias Shija, Uyui.
 
Wafanyabiashara wa kata ya Bukumbi wilaya ya Uyui mkoani Tabora wamechanga kiasi cha Tsh. 3,400,000/= kwa ajili ya kukarabati jengo la kituo kidogo cha polisi cha kata hiyo.

Akizungumzia suala hilo katibu wa umoja wa wafanyabiashara hao Maziku Kanati amesema fedha hizo zimetumika kukarabati jengo hilo ili kuimarisha ulinzi katika kukabiliana na matukio ya mara kwa mara ya uhalifu katani humo.

Amesema ongezeko la matukio ya uhalifu dhidi ya watu na mali zao yamepelekea wafanyabiashara hao kujitoa kwa hali na mali kukarabati jengo hilo ili liwe na sifa zinazokubalika na kuwawezesha polisi kutimiza majukumu yao kikamilifu.

Kanati amebainisha kuwa hali hiyo itawasaidia kudumisha amani na utulivu wakati wakijishughulisha na shughuli mbalimbali za kijamii na uzalishaji mali.

Naye mwenyekiti wa wafanyabiashara hao Jonas Mheza amesema kuimarika kwa kituo hicho cha polisi kutasaidia kuongezeka kwa askari wanaotoa huduma katika maeneo yao.

Aidha amesema matukio ya kihalifu katani humo yamekuwa yakitokea mara kwa mara hali inayowasababisha baadhi ya wafanyabiashara kuwa na hofu kufanya uwekezaji wenye tija.

Mwenyekiti huyo amewataka wafanyabiashara na wananchi wa kata ya Bukumbi kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi katika kuwafichua wahalifu ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Hata hivyo baadhi ya wakazi wa kata hiyo wamemuomba kamanda wa polisi mkoa wa Tabora kuwaondoa askari waliowahi kufanya kazi katika kituo hicho siku za nyuma kwa kuwa hawana rekodi ya uadilifu katika kutekeleza majukumu yao.

No comments: