Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, December 20, 2015

HOSPITALI YA KITETE INAKABILIWA NA UPUNGUFU WA DAMU SALAMA



Na Paul Christian, Tabora

Hospitali ya rufaa ya mkoa wa Tabora Kitete inakabiliwa na upungufu wa damu salama hali inayohatarisha maisha ya wagonjwa wanaohitaji huduma hiyo.

Akizungumzia hali hiyo meneja wa maabara ya hospitali hiyo Abdallah Haruna alisema mahitaji  halisi ni wastani wa Unit 15 hadi 20 kwa siku lakini kwa sasa wanapokea wastani wa Unit 5 kwa siku kutoka Benki ya damu salama kanda ya Magharibi.

Alisema hali hiyo imekuwa ikiwasababisha kugawanya mara mbili damu salama  iliyomo kwenye mfuko mmoja wenye ujazo wa mililita 500 kwa lengo la kuwahudumia wagonjwa wawili kwa wakati mmoja.

Abdalla amebainisha kuwa njia nyingine wanayoitumia kukabiliana na hali hiyo ni ndugu wa wagonjwa kujaza fomu maalumu na kujitolea damu.

Alibainisha kuwa hali huwa mbaya zaidi pale wanapokuwa na mgonjwa anayehitaji kuongezewa damu kutoka katika kundi O hasi ambalo linawatu wachache sana.

Meneja huyo wa maabara alisema tabia ya kundi la damu O hasi linaweza kumuongezea mtu yoyote lakini mtu mwenye kundi O hasi akihitaji damu ni lazima aongezewe na mtu mwenye kundi kama hilo tu.

Afisa tawala na utumishi wa Mpango wa Damu Salama kanda ya Magharibi Ludovick Mlay alikiri kuwepo kwa upungufu wa damu salama katika hospitali ya Kitete kutokana na kushuka kwa uchangiaji damu kwenye Mpango.

Alisema sababu mojawapo ya kushuka kwa uchangiaji huo ni kukosekana maandalizi ya kutosha ya kuuendesha Mpango wa damu salama mara baada ya ufadhili wa Marekani kufikia ukomo mwezi Mei mwaka huu.

Mlay alibainisha kuwa serikali  iliziagiza halmashauri za wilaya nchini kubeba jukumu la kukusanya damu kutoka kwa wananchi na kisha kuipeleka benki ya damu kwa ajili ya vipimo ili kubaini vimelea vya homa ya Ini B na C,Kaswende na Virusi vya UKIMWI.

Afisa tawala huyo alieleza kuwa halmashauri nyingi katika mikoa ya Tabora, Kigoma, Singida na Katavi  hazijaanza kutekeleza zoezi hilo kwa madai ya kutokuwa na fedha.

Alisema, “kutokana na utaratibu wa sasa halmashauri zinatakiwa kukusanya damu asilimia 80 ya mahitaji yote huku asilimia 20 inayobaki inakusanywa na Benki ya damu Salama.”

Mlay  alibainisha kuwa benki ya damu salama yenye makao yake mjini Tabora inatakiwa kukusanya unit 500 kwa mwezi sawa na wastani wa Unit 18 kwa siku.

Aidha alitaja sababu nyingine zinazozorotesha  zoezi la uchangiaji damu kuwa ni uuzwaji wa damu salama kwenye hospitali na vituo vya afya badala ya kutolewa bure pamoja na urasimu wakati wa kutoa huduma.

Mlay alieleza kuwa kundi la wanafunzi wa sekondari na vyuo ndilo linalotegemewa sana kuchangia damu na kwamba inapofika miezi ya likizo makusanyo ya damu hushuka.

Hata hivyo alionesha kuwa na matumaini kuwa utaratibu mpya wa ukusanyaji damu kupitia halmashauri utaongeza makusanyo na kuondoa tatizo la upungufu wa damu Salama.

Mahitaji  ya damu Salama kanda ya Magharibi ni wastani wa unit 67,000 kwa mwaka ambayo zaidi inahitajika kuokoa maisha ya watoto wenye umri chini ya miaka mitano, akinamama wajawazito, operesheni na wagonjwa wa ajali.

Benki ya damu salama kanda ya Magharibi ilianza shughuli zake mwaka 2007 na inahudumia mikoa ya Tabora,Kigoma,Katavi na Singida.
                        





No comments: