Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, December 30, 2015

WANANCHI WATAKA MIPAKA YA HIFADHI IWEKWE NA KUONEKANA



Na Hastin Liumba,Kaliua

WAKAZI wa kata ya Zugimlole wilaya ya Kaliua mkoani Tabora wameshangazwa na hatua ya maofisa wa maliasili kuwazuia kufanya shughuli za kilimo katika maeneo yanayodaiwa ni sehemu ya hifadhi  ya Mpanda Forest na Sawima.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakazi wa Kitongoji cha Kanyanya, kijiji cha Imbulisiasi pamoja na kitongoji cha Iga kijiji cha Uyumbu walisema hatua hiyo imeathiri uzalishaji wa chakula na hivyo kuwaweka kwenye hatari ya kukumbwa na njaa.

Wakazi hao walibainisha mazao ya chakula waliyolima katika maeneo hayo kuwa ni mahindi na mpunga kabla ya kutakiwa kusitisha shughuli hizo tarehe 12 mwezi huu. 

Aidha walieleza kuwa maofisa wa maliasili waliwanyang’anya zana zao za kilimo jambo linalowafanya washindwe kufanya shughuli za kilimo kwenye maeneo mengine.

Mmoja wa wakazi hao Peter Luhimba alisema serikali imeshindwa kuainisha mipaka ya hifadhi hizo jambo linalowachanganya na kushindwa kuelewa mipaka halisi ni ipi ili waiheshimu tofauti na ilivyosasa.

Sai Juma alibainisha kuwa wao kama wananchi ni sehemu ya uhifadhi wa hifadhi hizo hivyo wanapaswa kuijua mipaka pamoja na kushirikishwa ipasavyo katika ulinzi badala ya kuchukuliwa kama waharibifu.

Naye Leonard Charles alieleza kwamba hali ya kutokuwepo kwa mipaka ya wazi kwenye hifadhi hizo kunawafanya baadhi ya watumishi wa maliasili kuwaonea na kuwanyanyasa wananchi kwa lengo la kujinufaisha.

Kwa kauli moja wakazi hao wameiomba serikali kuangalia uwezekano wa kuwaruhusu wahudumie mazao yao hadi yatakapo komaa  na kuvunwa ambapo watatafuta  maeneo mengine yanayofaa kwa kilimo.

wameztaja zana zao za kilimo zilizochukuliwa na maafisa hao wa maliasili kuwa ni pamoja na majembe ya mkono, matrekta na ng’ombe wanao kokota majembe ya kilimo.

Diwani wa kata ya Zugimlole Balikeka Ramadhan alipohojiwa kuhusu suala hilo alisema wananchi wake sasa hawalimi baada ya kunyang’anywa zana za kilimo.

Diwani huyo alisikitishwa na maofisa hao wa maliasili kufika katika maeneo hayo yanayodaiwa yako ndani ya hifadhi bila kushirikiana na uongozi wa kata hiyo.

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Kaliua Athuman Kihamia alisema
zoezi hilo halikufanywa na maofisa wa ofisi yake bali lilifanywa na wakala wa misitu nchini TSF.

Alipohojiwa Mkuu wa wilaya Kaliua Hadijah Nyembo alisema naye alisema zoezi hilo la kuwahamisha wananchi wanaodaiwa kuwa ndani ya hifadhi wahusika ni Maliasili hivyo wakiulizwa watakuwa na majibu ya msingi.

Meneja misitu wa wilaya ya Kaliua John Madohora alisema wananchi hao
ni kweli wameingia na kuvuka mipaka ya hifadhi na wanaendesha kilimo.

Madohora alisema tumekuwa tukiwaondoa kisheria na kwamba tatizo kubwa lipo kwa wenyeviti wa vijiji na vitongoji kwani wamekuwa wakichukua fedha na kuuza maeneo ya hifadhi.

Aliyataja maeneo ambayo wananchi wamevamia ni Mpanda Line kwenye maeneo ya Kangeme, Lumbe, Usinge, Ukumbisiganga na Kakole na kwamba zipo taratibu za kuangalia mipaka na kwaleza wazi kuwa wako kwenye hifadhi.

Alisema alama za mipaka zipo na zinaonekana bayana na kumekuwa na jitihada za kufyeka nyasi ili ziweze kuonekana kwa uwazi.

Madohora alisema wanasiasa wanaingilia kati kuwatetea wananchi waendelee kukaa kwenye hifadhi  lakini mamlaka inachukua hatua hizo kunusuru misitu.

WATAKAOSHINDWA KUWAPELEKA WATOTO WAO SHULE KUKUTANA NA MKONO WA SHERIA.


Mkuu wa wilaya ya Tabora Suleiman Kumchaya akiwahutubia wakazi wa kijiji cha Kapunze,kata ya Ikomwa

 
Na Paul Christian, Tabora.


Wazazi na walezi wa wilaya ya Tabora wametakiwa kuwapeleka watoto wao shule na endapo watashindwa kufanya hivyo watachukuliwa hatua za kisheria.

Mkuu wa wilaya ya hiyo Suleiman Kumchaya ametoa agizo hilo Jumanne jioni alipokuwa akiwahutubia wakazi wa kijiji cha Kapunze katika kata ya Ikomwa wilayani humo.

Amesema serikali ya awamu ya tano inatoa elimu bure kuanzia darasa la awali hadi kidato cha nne na kwamba wazazi au walezi hawapaswi kuchangia fedha yoyote.

Mkuu huyo wa wilaya ya Tabora amewataka wazazi na walezi wenye watoto wenye umri wa miaka kati ya minne na mitano kuwapeleka kuandikishwa kwa ajili ya kuanza darasa la awali mapema mwaka ujao.

Aidha amesisitiza watoto wenye umri wa miaka sita waandikishwe   darasa la kwanza na kwamba zoezi hilo halipaswi kutozwa fedha.

Kumchaya amesema kwa kuwa jukumu la kutoa elimu bure kuanzia elimu ya awali hadi kidato cha nne liko mikononi mwa serikali hakuna sababu ya mtoto kushindwa kufika shule na kusoma.

Amebainisha kuwa serikali imechukua jukumu la kugharamia madawati, vifaa vya michezo,chakula kwa wanafunzi wa bweni,ujenzi wa miundombinu ya shule ikiwemo vyumba vya madarasa na nyumba za walimu.

Mkuu huyo wa wilaya amesema jukumu la wazazi na walezi ni kuwapatia watoto wao  sare za shule na michezo, vifaa vya kujifunzia kama vile kalamu na madaftari, nauli za kuwasafirisha watoto wao wanapotoka na kurudi shule wakati wa likizo.

Aidha kumchaya ameonya kuwafukuza kazi walimu  watakaobainika kuomba fedha wakati wa kuwaandikisha watoto kujiunga darasa la awali, la kwanza pamoja na kidato cha kwanza.

Ametoa wito kwa wazazi na walezi wilayani humo kutotoa fedha  na endapo watatakiwa kufanya hivyo watoe taarifa ili hatua za kinidhamu zichukuliwe.




WATENDAJI WA SERIKALI WATETEE MASLAHI YA NCHI BADALA YA KUMFURAHISHA DKT.MAGUFULI



Bwana Samson Amos akifafanua jambo

 
Na Paul Christian, Tabora.

Viongozi wa serikali wameshauriwa kuwa makini wakati wa kutoa matamko au kuchukua hatua za kiutendaji wakati huu wa kaulimbiu ya hapa kazi tu.

Ushauri huo umetolewa na mshauri wa tiba mbadala wa bidhaa za Tiens mjini Tabora Samson Amosi katika mahojiano maalum na mwandishi wa Tabora Watch Blog.

Amesema kauli ya serikali ya hivi karibuni ya kusitisha matangazo ya wataalam wa tiba mbadala kwenye vyombo vya habari pamoja na kuweka masharti ya kuhariri matangazo hayo kabla ya kwenda hewani inapaswa kutekelezwa kwa umakini ili kutenda haki.

Samson amesema, “kama lengo ni kudhibiti ubora wa bidhaa, huduma au utaalamu wa tiba mbadala itakuwa vyema tukiona juhudi hizo katika matangazo ya vileo, sigara na uzalishaji wa tumbaku bidhaa ambazo zinamadhara ya wazi kwa afya za walaji.”

Amebainisha kuwa baadhi ya bidhaa zinazotumiwa kwenye  tiba mbadala zimetengenezwa kwa virutubisho na madini kama chakula cha ziada kwa watu waliokosa na kusababisha miili yao kushambuliwa na magonjwa mbalimbali.

Samson amesema bidhaa hizo zimetengenezwa baada ya kufanyiwa utafiti wa kina uliothibitisha kufanya kazi kwa ufanisi zaidi kuliko hata dawa zinazotumiwa hospitalini ambazo nyingi zinamadhara kwenye miili licha ya kutibu.

Mshauri huyo wa tiba mbadala amefafanua kuwa  watendaji wa serikali wasitekeleze majukumu yao kwa kumfurahisha Rais John Pombe Magufuli  bali wafanye hivyo kwa kuwa ni wajibu wao wa kulinda na kutetea maslahi ya taifa.

Samson amesema sekta ya afya inahitaji uwekezaji wa maarifa na ufahamu wa hali ya juu katika ugunduzi wa dawa za asili zenye uwezo wa kutibu magonjwa ambayo hayatibiki katika hospitali za mfumo rasmi.

Amefafanua kuwa taifa linapaswa kuwekeza kwenye tafiti zitakazotoa majibu sahihi ya tiba za magonjwa sugu badala ya kubeza na kukumbatia dawa zilizogunduliwa na wataalamu wa mataifa mengine .

Aidha amesema kuwa licha ya kutoa ushauri wa tiba mbadala amekuwa akilipia leseni yake ya biashara shilingi 80,000/= , kodi ya mapato shilingi 200,000/= pamoja na kodi ya pango shilingi 1,200,000/= kwa mwaka hali, inayoonyesha uhalali katika shughuli anazozifanya.

Samson ameongeza kuwa Mamlaka ya Chakula na Dawa TFDA kanda imeagiza kuanza kulipwa shilingi 60,000/= kwa mwaka jambo linaloongeza mzigo mwingine kwa washauri wa tiba mbadala ambao wanatekeleza majukumu yao kwa kamisheni.

Amesisitiza kuwa licha ya Tanzania kuwa na mimea na vitu vingine vya asili wataalamu wake wameshindwa kushirikiana na kugundua dawa, virutubisho au madini kupitia mimea hiyo  kwa lengo la kuzalisha bidhaa za kitanzania  kama zilivyo nchi za Mashariki ya mbali.

HALMASHAURI YA WILAYA YA UYUI YAVUNJA MKATABA NA KAMPUNI YA SARAM


Na Halima Ikunji ,Tabora. 
Halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoani Tabora imevunja mkataba wa ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje OPD katika hospitali ya wilaya hiyo kufuatia Mkandarasi kampuni ya SARAM kukiuka masharti ya mkataba huo.

Akizungumza na waandishi wa habari mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Hadija Makuwani amesema kampuni hiyo ya jijini Dar es Salaam imesitisha shughuli za ujenzi wa OPD hiyo iliyopo Isikizya makao makuu ya wilaya hiyo.

Amesema mkandarasi huyo amesimamisha shughuli za ujenzi kwa muda wa miezi 9 na hivyo kwenda kinyume na kifungu namba 62.2 cha mkataba huyo.
Hadija ameeleza kuwa mkandarasi huyo pia alikiuka vifungu namba 10.1 na 10.2 vya mkataba huo kwa kumtumia mtaalamu ambaye hatambuliki kwenye mkataba huo.

Mkurugenzi huyo mtendaji ametaja sababu nyingine zilizosababisha kuvunjwa kwa mkataba huo ni mkandarasi huyo kushindwa kuhudhuria vikao vya kazi vilivyoitishwa na msimamizi wa mradi huo jambo ambalo ni kinyume na kifungu namba 35.2 cha mkataba huo.

Hadija amebainisha kuwa hatua za kuvunja mkataba huo zimezingatia kifungu cha 62.1 ambacho kinamtaka mwajiri au mkandarasi kuvunja mkataba endapo mmoja kati yao atashindwa kutimiza masharti ya mkataba huo.

Aidha amefanunua kuwa wakati mkataba unavunjwa mkandarasi huyo alikuwa ametekeleza kazi yenye thamani ya sh. 138,109,468.86 na madai
anayostahili ni sh. 3,564,245.59 kama malipo ya kazi.

Hadija amekiri kuwa  kiasi cha sh.5,650,157.95 kama malipo ya kinga iliyokuwa imekatwa kwenye hati alizokwishalipwa na kuongeza kuwa malipo ya fedha hiyo atalipwa baada ya tathmini ya mwisho.

Mkurugenzi huyo amebainisha kuwa gharama za mkataba wa kazi hiyo ilikuwa sh 299,654,364.60 huku nyongeza ikiwa ni sh 15,257,200.00 jambo linalofanya gharama ya mradi wote kuwa kiasi cha sh 314,911,564.60.

“mkataba huo umevunjwa rasmi tarehe 22 mwezi huu baada ya kujiridhisha pasipo shaka kuwa mkandarasi ameshindwa kutimiza matakwa ya kisheria ya mkataba wake’, alisema Mkurugenzi.

Hivi karibuni Halmashauri ya wilaya ya Kaliua mkoani Tabora ilisitisha mkataba na kampuni hiyo ya ujenzi kwa madai ya kukiuka mkataba wa ujenzi wa ofisi ya mkurugenzi, jengo la wagonjwa wa nje OPD, nyumba za watumishi, jengo la maonesho katika eneo la Ipuli mjini Tabora.