Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Saturday, February 20, 2016

WALALAMIKAJI KESI YA UCHAGUZI JIMBO LA TABORA MJINI WATAKIWA KUJIBU HOJA ZA WALALAMIKIWA




Na, Murugwa Thomas, Tabora.

Mahakama kuu kanda ya Tabora imeahirisha shauri la kupinga matokeo ya uchaguzi  wa ubunge jimbo la Tabora mjini  yaliyompa ubunge Emanuel Mwakasaka wa Chama Cha Mapinduzi CCM hadi Jumatatu  Februari 22 mwaka huu.

Shauri hilo  namba 3/2015 limeahirishwa  kutokana na mawakili wa upande wa walalamikaji  Hashimu Mziray  na Job Kiraria  kushindwa kujibu hoja za wajibu maombi zilizowasilishwa Mahakamani hapo na mawakili Juma Masanja na Kamaliza Kayaga.

Kwa upande wao wajibu maombi waliwasilisha pingamizi Mahakamani hapo wakitaka shauri hilo liondolewe kwa vile walalamikaji  hawakuwa na sababu za msingi kufungua kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi huo.

Akiahirisha kesi hiyo  jaji wa Mahakama kuu kanda ya Tabora Leilla Mgonya amewataka mawakili wa walalamikaji wawe wamejibu hoja za pingamizi za wajibu maombi kufikia jumatatu ijayo  na kuonya kutoacha kufika mahakamani.

Amesema kuwa mahakama kuu imejiwekea utaratibu kwamba kesi zote zinazohusu uchaguzi zinapaswa kumalizika na kutolewa uhamuzi si zaidi ya mwezi Machi mwaka huu.

 Katika shauri hilo wanachama wanne wa  Chama Cha Wananchi CUF  Jumanne Mtunda, Johari Kassanga, Shaban Mussa na Thomas Ayengo walifungua kesi Mahakama kuu kupitia kwa wakili wao Mziray wakipinga uchaguzi uliofanyika na kumpa ushindi Emanuel Mwakasaka wa CCM kwamba haukuwa huru na wa haki.

Awali waleta maombi  hao wanaopinga uhalali wa mbunge huyo wa CCM kushinda uchaguzi huo  waliomba Mahakama kupanga tarehe nyingine  ya kuendelea na shauri hilo  kwa madai kwamba mawakili wao hawakufika kutokana na majukumu mengine.

Hoja ambazo hawajajibu ni pamoja na kuwasilisha ushahidi na vielelezo  vya kupinga matokeo hayo  ikiwemo kwamba mlalamikiwa wa kwanza alitoa rushwa  ndipo akaweza kupigiwa kura wakati wa uchaguzi mkuu uliopita.


No comments: