Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Friday, February 5, 2016

MAGRETH SITTA AULIZA SWALI BUNGENI KUHUSU TUMBAKU, JE MAJIBU YA SERIKALI YANARIDHISHA?



 
MAGRETH SIMWANZA SITTA
Na Paul Christian.

Katika kipindi cha Maswali na Majibu leo Bungeni mjini Dodoma, mbunge wa Urambo Mheshimiwa Magret Simwanza Sitta ameuliza swali la msingi lifuatalo.

Mfumo wa sasa wa kuwahudumia wakulima wa zao la Tumbaku wa wilaya ya Urambo na mkoa wa Tabora kwa ujumla unamapungufu mengi unaowaletea wakulima usumbufu kama vile bei ya pembejeo kuwa kubwa kutokana na kuagizwa nje, riba kubwa za benki, masoko ya Tumbaku kutokuwa na uhakika na hatimaye kusababisha kushuka thamani, Je ni kwa nini hasara inayotokana na matatizo hayo ibebwe na mkulima peke yake?

Akijibu swali hilo la Msingi Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi William Ole Nasha amesema, “Naibu spika, serikali inakubaliana na mheshimiwa mbunge yapo maeneo mbalimbali yanayomkosesha mkulima mapato, maeneo hayo ni pamoja na mfumo wa usambazaji pembejeo uliokuwa na mianya mingi unaosababisha madeni hewa, baadhi ya viongozi wa vyama kukopa fedha nyingi kupita uwezo wa vyama kuzalisha Tumbaku na kadhalika. 

Kwa sasa serikali Imebadili mfumo huo na kuelekeza wagavi wa pembejeo hizo kuzifikisha moja kwa moja kwenye vyama vya msingi tofauti na utaratibu wa awali wa kupitisha pembejeo kwenye vyama vikuu.”
“Aidha ili kuwa na uhakika wa soko kilimo cha Tumbaku nchini uendeshwa kwa mkataba kati  ya wanunuzi na wakulima, hivi sasa bei upangwa kabla ya msimu kilimo kuanza ili mkulima ajue bei na kiasi ambacho mkulima anatakiwa kuzalisha.”

“Tatizo la soko na bei mara nyingi uwakumba wale wakulima wanaozalisha tumbaku bila kuwa na mikataba ambapo ujikuta tumbaku yao ikikosa soko au wakipewa bei ya chini.”

“Mheshimiwa Naibu Spika, serikali imeendelea kuchukua hatua za kukabiliana na changamoto zinazomkabili mkulima wa Tumbaku, hatua hizo ni pamoja na kuboresha mfumo wa upangaji wa bei ya Tumbaku ambapo wakulima hupendekeza bei yenye tija kwao na kuiwasilisha kwa wanunuzi kupitia vikao vya halmashauri ya Tumbaku yaani Tobacco Council, bei hiyo hujadiliwa na hatimaye kufikia muafaka.”

“Mfumo huu wa upangaji wa bei umeanza kutumika rasmi msimu wa 2015/2016 sanjari na maboresho ya mfumo huu serikali inaendelea na jitihada za kuongeza wanunuzi wa tumbaku kutoka China ili kuongeza ushindani kumuwezesha mkulima kupata bei nzuri.”

“Aidha serikali itapitia tozo za pembejeo zinazoingia nchini na kuangalia uwezekano wa kuziondoa ili kumpunguzia mkulima gharama za uzalishaji.”
 
TUMBAKU
Mheshimiwa Magret Simwanza Sitta ameuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

(a) “Mheshimiwa Naibu Spika Waziri amekiri kwamba mfumo uliopo unamatatizo katika kumuhudumia mkulima, lakini serikali inashiriki kikamilifu katika kupanga bei katika mfumo mzima, sasa kwa kuwa serikali inashiriki kwa kupitia wakala wake Bodi au Council, je serikali haioni kwamba inawajibika kubeba sehemu ya hasara anayopata mkulima?”

b) “Kwa kiasi gani mmefaulu kupata wanunuzi zaidi kutoka China ili soko liwe la haraka wakulima wanufaike?”

Akijibu maswali hayo ya nyongeza Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi William Ole amesema, “Tobacco Council au halmashauri ya Tumbaku inawakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya Tumbaku, serikali yenyewe haihusiki moja kwa moja katika kupanga bei lakini imeweka utaratibu ambao wadau wenyewe wanaweza kukaa kukutana kwa uhuru wao na kupanga bei hata hivyo serikali imechukua hatua mbalimbali za kuhakikisha kwamba bei za tumbaku zinaendelea kuwa nzuri.”

“Tunafahamu kwamba kuanzia mwaka 2013 Bunge hili lilipitisha Sheria mpya ya vyama vya Ushirika, utaratibu mpya wa vyama vya Ushirika ni utaratibu ambao pamoja na mambo mengine unawaruhusu wakulima wa mazao mbalimbali kuendesha shughuli zao kwa kuwa na uhuru zaidi, lakini vile vile mpango ule umeunda Tume ya Ushirika ambayo inakuwa karibu na vyama vya Ushirika ili kuweza kuondoa kero zilizopo tunafikiri utaratibu huu unaleta ufanisi zaidi katika kilimo cha Tumbaku na mazao mengine ikiwa ni pamoja na kusaidia suala la bei.”

“Lakini nitumie fursa hii kuwaeleza waheshimiwa wabunge pamoja na changamoto nyingi zilizopo kwenye sekta ndogo ya Tumbaku, tunafikiri sekta ndogo ya Tumbaku ni eneo ambalo limeanza kuonyesha mifano ya kufanikiwa hii ni kwa sababu ndio sekta ndogo ya pekee ambayo mkulima anakuwa na uhakika wa kuuza zao lake tokea siku ya kwanza anapoanza kuweka mbegu shambani kwa sababu ni kilimo cha mkataba.”

“Kwa hiyo tukiondoa changamoto zilizopo tunafikiri ni eneo ambalo bado inawezekana  kupata mafanikio makubwa lakini vile vile tungependa kutumia usahihi kuwaeleza wakulima kuwafahamisha kwamba kufanikiwa kutumia kilimo cha mkataba unaweza kusaidia tu kama kila mtu ataheshimu mkataba.”

“Kwa mfano mwaka huu tayari wakulima wanafahamu inatakiwa wazalishe tumbaku kiasi gani, tunaomba wale ambao hawako kwenye mkataba wasizalishe tumbaku kwa sababu ukizalisha hautapata mnunuzi.”

Akijibu Kipengele (b) cha swali la nyongeza Naibu Waziri huyo amesema, “mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inajitahidi kuongea na wafanyabiashara kutoka China, tumefika hatua nzuri sana kinachobakia sasa ni wao kumaliza taratibu za nchini kwao ili nao waweze kuingia kwenye mfumo rasmi wa kununua Tumbaku ili kuondoa ukiritimba ambao mpaka sasa hivi nchi nzima kampuni zinazonunua Tumbaku ni nne tu.”

“Kwa hiyo tunafikiri kwamba kampuni zikiwa nyingi maana yake tutaondo Monopoly na hivyo bei itakuwa nzuri, Nashukuru.”

No comments: