JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE
NA WATOTO
TAMKO
KUHUSU MWENENDO WA UGONJWA WA KIPINDUPINDU NCHINI LILILOTOLEWA NA MHE. DR.
HAMISI A. KIGWANGALLA (MB); NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA,
WAZEE NA WATOTO, TAREHE 22 FEBRUARI 2016
Ndugu Waandishi wa Habari,
Taarifa hii ni mwendelezo wa utaratibu ambao Wizara imejiwekea kila wiki wa kutoa taarifa kwa umma
kuhusu hali ya kipindupindu nchini ikiwa
ni pamoja na kueleza juhudi mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa ili
kukabiliana na hali hii. Hadi kufikia tarehe 21 Februari 2016, jumla ya watu 16,352
wameugua ugonjwa huo, na kati yao watu 249 wamepoteza maisha.
Takwimu za wiki iliyopita zinaonyesha kuwa kuanzia tarehe 15 hadi 21
Februari 2016, idadi ya wagonjwa wapya walioripotiwa ni 499 ambapo kati yao
watu 6 walipoteza maisha. Idadi ya wagonjwa wiki hii imepungua japo sio kwa
kiwango kikubwa (5%) ukilinganisha na wiki iliyoishia tarehe 14 February ambapo
wagonjwa 528 waliripotiwa.
Jumla ya
mikoa ambayo imeripoti kuwa na wagonjwa kwa wiki iliyopita ni 11, ambapo Mkoa
wa Iringa ndio ulioongoza kwa kuripoti idadi kubwa ya wagonjwa yaani wagonjwa 143
(Iringa Vijijini 143) ukifuatiwa na Mwanza 94 (Ilemela 50, Ukerewe 22,
Nyamagana 14, Sengerema 1), Mara 87 (Musoma mjini 38, Tarime vijijini 24, Rorya
19, Bunda 4 na Musoma vijijini 2), Dodoma 66 (Chamwino 25, Mpwapwa 23 na Dodoma
mjini 18) na Morogoro 42 (Morogoro Manispaa 22, Ulanga 13 na Kilosa 7). Mikoa
mingine iliyoripoti wagonjwa ni Mbeya 30, Arusha 17, Dar es Salaam 14, Simiyu
3, Kilimanjaro 2 na Manyara 1.
Ndugu Waandishi wa Habari,
Wizara
bado inaendelea kukumbana na changamoto mbalimbali katika kukabiliana na
ugonjwa wa kipindupindu. Vikosi kazi vya wataalamu kutoka wizara yangu wanaoendelea
kuzuru maeneo mbalimbali wameendelea kuibua changamoto hizo na kuhakikisha
zinafanyiwa kazi haraka iwezekanavyo ili kuzuia ueneaji wa vimelea vya ugonjwa
huu na kisha kuutokomeza kabisa.
Moja
ya changamoto kubwa inayoendelea kujitokeza ni pale ambapo baadhi ya wataalamu
wa ngazi mbalimbali pamoja na wanajamii wanapowaficha wagonjwa na hivyo kutoa
taarifa ya wagonjwa wachache kuliko uhalisia.
Madhara yanayoambatana na hili ni
kutokuwepo kwa taarifa za kutosha zitakazoongoza juhudi za kuzuia ugonjwa kutoka
katika maeneo ambayo wagonjwa hawakutolewa taarifa na hivyo kuongeza hatari ya
ugonjwa kuendelea kusambaa kimya kimya na baadae kusababisha wagonjwa wengi
kujitokeza katika maeneo hayo kwa mara moja.
Wizara
inaendelea kufanya juhudi mbalimbali kuhakikisha kuwa inatokomeza ugonjwa huu
wa kipindupindu na inazitaka mamlaka zinazohusika na kuwatambua wagonjwa kushirikiana
na kutoa taarifa sahihi kama inavyoelekezwa katika miongozo mbalimbali ya
Wizara ikiwamo muongozo wa udhibiti wa magonjwa ya milipuko Tanzania wa mwaka
2011 “IDSR” na muongozo wa udhibiti wa ugonjwa wa kipindupindu toleo la tatu wa
mwaka 2015.
Pia kwa jamii tunawasihi pale wapatapo wagonjwa wawapeleke katika
vituo vyetu vya kutolea huduma ili wapatiwe matibabu sahihi na kutolewa
taarifa. Kwa kufanya hivyo taarifa za kutosha na sahihi zitakazosaidia
kupambana na kuutokomeza ugonjwa huu zitapatikana kwa wakati na hivyo kuwezesha
kuutokomeza ugonjwa huu mapema.
Tunatoa rai kwa viongozi hususani ngazi ya
Mikoa na Wilaya kutokutoa kauli za kutaka kuwaadhibu watendaji na viongozi wa
ngazi za chini kwa kigezo cha wagonjwa kuwepo katika maeneo yao kwani kwa
kufanya hivyo wataongeza kasi ya kuficha wagonjwa na hivyo kukwamisha juhudi za
kupambana na kipindupindu.
Aidha tunatoa wito kwa mikoa yote nchini kuhakikisha
kuwa wanaimarisha vikao vya Kamati za Afya ya Msingi (PHC meetings) na kutumia
taarifa zinazotokana na uchambuzi wa mwenendo wa ugonjwa katika maeneo yao ili ziwasaidie
kupanga mbinu sahihi za udhibiti wa kipindupindu.
Ndugu waandishi wa habari,
Tarehe
15 Februari 2016 nilitembelea kijiji cha Mboliboli kata ya Pawaga Wilaya ya
Iringa ambacho kilikumbwa na mafuriko
kutoka mto Ruaha yaliyotokana na mvua
kubwa kunyesha na maji kuzoa vyoo ambavyo vilitapanya kinyesi katika vijiji
vilivyopo kando ya mto uliosababisha mlipuko wa Kipindupindu.
Sambamba na hilo
Wizara ilituma timu ya wataalamu ili kufanya tathmini na kuongeza nguvu ya
kupambana na kuzuia ueneaji wa ugonjwa huu kwa wahanga wa mafuriko.
Tunaupongeza
Mkoa wa Iringa pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kwa juhudi
wanazoziendeleza za kuutokomezwa ugonjwa huu na kuuzuia usisambae katika maeneo
ya jirani.
Wizara kwa kushirikiana na
wadau mbali mbali itaendelea kutoa msaada wa kitaalamu kwa Mikoa na Halmashauri
zote ili kusaidia juhudi zilizopo za kupambana na ugonjwa huu na hatimaye
kuutokomeza kabisa.
Tunaendelea
kuisihi jamii kuungana na halmashauri, mikoa pamoja na wizara katika juhudi za
kupambana na ueneaji wa kipindupindu kwa kuzingatia yafuatayo:
- kunywa
maji yaliyo safi na salama
- kuepuka
kula chakula kilichoandaliwa katika mazingira yasiyo safi na salama
- kunawa
mikono kwa sabuni na maji safi
yanayotiririka.
- kutumia
vyoo wakati wote na kutokujisaidia ovyo katika vyanzo vya maji vya mito, maziwa
na mabwawa.
- Kutokutiririsha
maji taka na vinyesi ili kuepuka uchafuzi wa vyanzo vya maji.
Pia wananchi wanahimizwa kuwahi mapema katika vituo
vya kutolea huduma za afya mara waonapo dalili kuu za ugonjwa wa kipindupindu
ambazo ni pamoja na kuanza ghafla kuharisha mfululizo kinyesi cha majimaji na kunako
weza kuambatana na kutapika, kulegea, kusikia kiu, midomo kukauka, na kuishiwa
nguvu.
Mgonjwa anaweza kupoteza maisha endapo hatapata huduma yoyote ya tiba
katika muda mfupi na hasa kutokana na kuishiwa maji.
Ndugu Waandishi wa Habari,
Wizara
pia inapenda kuwajulisha wananchi wote
kwa ujumla kuhusu juhudi ambazo serikali imezichukua kama hatua za awali za
kujiandaa kuzuia maambukizo ya ugonjwa wa homa ya Zika ambao Mheshimiwa Ummy A. Mwalimu (Mb), Waziri wa Afya
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto alishautolea taarifa hapo awali.
Wizara imeanza kutekeleza mikakati mbalimbali ya kusaidia kuiweka nchi katika
hali ya utayari kupambana na tishio la ugonjwa wa homa ya Zika, Mikakati hiyo
ni pamoja na:
1. Kuimarisha
ufuatiliaji wa utambuzi wa watoto waliozaliwa na vichwa vidogo (microcephaly)
kupitia hospitali zote za Rufaa kwa kutumia mfumo wa ufuatiliaji wa ugonjwa wa
Rubella ambayo inaendelea. Aidha takwimu za watoto waliozaliwa na vichwa vidogo
ambazo zimekwisha kukusanywa kwa kupitia mfumo huu zinaendelea kuchambuliwa kwa
uhakika ili kuona kama lipo tishio la ongezeko la ulemavu wa aina hii nchini.
2. Sampuli
za wagonjwa wanaojitokeza na homa na kukidhi vigezo vya Zika Virus wanaotolewa
taarifa na mfumo huu zitakusanywa na kupimwa katika maabara zilizopo kwenye
kituo cha utafiti kilichopo KCMC Moshi “KCRI”.
3. Kufanya
uchunguzi kwa mbu waliokusanywa wakati wa Dengue na kuona iwapo wana virusi hivyo
na pia kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji wa magonjwa yaambukizwayo na mbu kwa
ujumla (Entomological Surveillance) ili kuweza kuiwezesha Serikali kutambua
kama kuna viashiria vya virusi hivyo kuwepo katika jamii ya mbu.
4. Kuimarisha
mfumo wa ufuatiliaji wa magonjwa kwa baadhi ya maeneo yenye kuwa na wagonjwa wa
homa (Acute Febrile Illness Sentinel Surveillance) ili kubaini kama virusi hawa
ni sehemu ya vimelea vinavyowasababishia homa au la.
5. Mwisho
Wizara inaandaa Mpango kazi wa namna ya kukabiliana na Zika ambao utakamilika
katika kipindi cha wiki moja ijayo.
Hitimisho
Wizara
inaendelea kutoa rai kwa jamii, wataalamu na viongozi katika ngazi zote kwamba kila
mmoja wetu atimize wajibu wake katika harakati za kuudhibiti ugonjwa wa
Kipindupindu.
Kwa
mara nyingine tena tunaendelea kuwashukuru wadau wote, yakiwemo Mashirika ya
Kimataifa kwa mchango wao mkubwa katika jitihada zetu za kupambana na magonjwa.
Aidha tunawashukuru na kuwapongeza watumishi wa afya katika ngazi mbali mbali
kwa juhudi zao katika kupambana na
ugonjwa huu.
Pia tunawapongeza waandishi wa habari kwa kuendelea
kuisaidia Serikali kuielimisha jamii jinsi ya kujikinga na kipindupindu
kusambaza taarifa mbalimbali zinazotolewa na Wizara yangu kwa ngazi zote
zinazohusika kwenye mapambano ya Kipindupindu.
Nawashukuru
kwa kunisikiliza
No comments:
Post a Comment