Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Tuesday, February 23, 2016

KESI YA KUPINGA MATOKEO YA UCHAGUZI JIMBO LA TABORA MJINI, UAMUZI WA KUSIKILIZA SHAURI LA MSINGI KUTOLEWA IJUMAA



Na, Murugwa Thomas,Tabora

UAMUZI wa kusikilizwa shauri mama la kupinga matokeo ya uchaguzi wa
Ubunge jimbo la Tabora mjini utatolewa Ijumaa tarehe 26 Februari, 2016 baada ya mahakama kupokea majibu ya mapingamizi yaliyowasilishwa na
walalamikaji.

Hatua hiyo imefikiwa Jumatatu na jaji Leila Mgonya wa mahakama kuu kanda ya Tabora baada ya wakili wa wadai Job Keraria kujibu kwa majibishano badala ya maandishi  mapingamizi yaliyowasilishwa na mawakili Kamaliza Kayaga na Juma Masanja wanaowawakilisha wadaiwa.

Awali jaji Mgonya alisema kuwa amekubali kupokea kwa majibishano
majibu ya mapingamizi hayo kutokana na kuzingatia misingi ya haki ili
maamuzi ya shauri hilo yaweze kutolewa mapema kama serikali
ilivyoelekeza.

Jaji mgonya alishangaa kuona mawakili wa waleta maombi kutochukulia
uzito madai yao kutokana na kitendo chao cha kuzembea kujibu hoja za
mapingamizi zilizowasilishwa na wajibu maombi kwa maandishi kama
walivyoelekezwa.

“Inaonekana walalamikaji walioleta shauri hili mahakamani
hawalichukulii katika uzito unaostahili”  alisema jaji Mgonya.

Kufuatia hali hiyo wakili Kayaga alidai kwamba kutokana na  waleta
maombi kushindwa kutekeleza amri ya mahakama iliyo tolewa tarehe 25
Januari mwaka huu  basi inaonekana hawana majibu hivyo  usikilizwaji uendelee .

Katika mapingamizi yao  wakili Kayaga alidai mahakamani hapo kuwa
walalamikaji ambao ni wapiga kura hawana haki kisheria kupinga matokeo ya uchaguzi mahakamani kwa vile haki yao haikudhulumiwa.

Naye  wakili Masanja anayemwakilisha mwanasheria mkuu wa serikali na
msimamizi wa uchaguzi  alidai kwa vile walalamikaji walishiriki uchaguzi
na waliweza kupiga kura  hawana madai yoyote  kwa wateja wake.

Wakili  Keraria alipinga hoja hizo na kusema kwamba walalamikaji wanayo haki kama raia  zinazolindwa na sheria za nchi pamoja na kuzingatia matakwa ya katiba ambayo ndiyo sheria mama.

Wanachama wanne wa Chama Cha Wananchi (CUF)  Jumanne Mtunda, Johari Kassanga, Shaban Mussa na Thomas Ayengo   kupitia kwa wakili wao wanaiomba mahakama itengue matokeo ya uchaguzi huo uliompa ushindi  Emanuel Mwakasaka wa CCM kwa madai  haukuwa huru na wa haki.

Madai mengine ni  kwamba mlalamikiwa wa kwanza alitoa rushwa  ndipo
akaweza kupigiwa kura wakati wa uchaguzi mkuu uliopita na kufanikiwa
kushinda.

No comments: