Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Tuesday, March 1, 2016

WATOTO YATIMA NA WA MAZINGIRA DUNI WAISHUKURU SERIKALI YA JAPANI


PICHA KUTOKA MAKTABA
Na Halima Ikunji,Uyui.


Watoto yatima na wanaoishi katika mazingira duni 159 katika kata za Ilolangulu na Isila wilaya ya Uyui mkoani Tabora,wameishukuru Serikali ya Japan kwa kuwasaidia kupata majengo mawili ya kituo cha kulelea watoto hao.

Wakizungumza na waandishi wa habari katika sherehe fupi ya kukabidhi mradi wa ujenzi wa kituo hicho kilichojengwa kijiji cha mbola kilichopo kwenye mradi wa vijiji vya milenia, wamesema mradi  huo kupitia ufadhili wa serikali ya Japan umewanufaika katika sekta mbalimbali ikiwemo miradi ya maji, elimu na afya.

Watoto hao wamebainisha kuwa wazazi wao walifariki kwa magonjwa mbalimbali na kuwaacha wakiwa wadogo ambapo  walezi wao katika familia hawakuwa na uwezo wa kuwatunza hali iliyowasababisha kuwa  ombaomba,vibaka na wengine kufanya ukahaba ili wajipatie chakula.

Awali katika sherehe hizo mratibu wa mradi wa vijiji vya milenia Dkt, Grerson Nyadzi amesema kuwa kituo hicho kimejengwa kwa muda wa miezi 10 kuanzia mwezi Mei mwaka uliopita na umegharimu zaidi ya Tsh. Mil 176.

Nyadzi amebainisha kuwa licha ya kukamilika kwa majengo hayo mawili bado kunahitajika  vitanda, magodoro, vyandarua,  jiko la kupikia chakula na vifaa vya ofisini hivyo ameiomba Serikali ya Tanzania iweze kuunga mkono juhudi hizo.

Mratibu huyo amesema kuwa katika ujenzi huo jamii ilishirikishwa kwa kuchangia nguvu kazi yenye thamani ya Tsh. Mil. 12.9 ambapo wafadhili walichangia Tsh. Mil. 163,601,448 sawa na dola za kimarekani 91,4996. 

Nae Balozi mdogo wa Japan, Hiloyuki Kubota katika hotuba yake amesema  kuwa kituo hicho cha watoto hao kitakuwa na uwezo wa kupokea watoto wengine 96 ambao wanaishi katika mazingira magumu na wasio jiweza kiuchumi.

Balozi Kubota amebainisha kuwa Serikali ya Japan inalenga kusaidia maeneo hayo katika Jamii, kwani anaimani kwamba kituo hicho kitasaidia watoto hao kwa kuwapa mazingira bora na nafasi za kutimiza ndoto zao.

Aidha  Balozi huyo ameiomba halmashauri ya wilaya ya Uyui kutenga bajeti kwa ajili kwa ajili ya kuendesha wa kituo hicho.

No comments: