Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Saturday, March 26, 2016

BARAZA LA MADIWANI LADAIWA KUTUMIKA KISIASA KUHAMISHA MRADI WA MILIONI 100,004,000/-



REHEMA KABATA
Na Paul Christian,Tabora.

CHAMA Cha Wananchi CUF wilaya ya Tabora kimeitaka serikali ya mkoa wa Tabora kuingilia kati maazimio ya baraza la Madiwani wa halmashauri ya manispaa ya Tabora kuahamisha mradi wa ujenzi kutoka zahanati ya Town Clinic kata ya Chemchem na kuupeleka kata ya Ifucha.


Akizungumza na Tabora Watch Diwani wa kata ya Chemchem katika manispaa hiyo kwa tiketi ya CUF Rehema Kabata amesema baraza hilo la madiwani limetumia wingi wa madiwani wa chama tawala kupitisha maazimio yanayoathiri kata zinazongozwa na vyama vya upinzani.


Amesema Mradi huo wa ujenzi wa wodi ya wazazi pamoja na chumba cha kujifungulia akinamama wajawazito wenye thamani ya shilingi milioni 100,004,000 ulikuwa kwenye mkakati wa utekelezaji tangu mwaka wa fedha wa 2014/2015 hadi mwaka wa fedha 2016/2017  ulipopata fedha hizo.


Diwani Kabata amefafanua kuwa kikao cha madiwani wa halmashauri hiyo kilichoketi  Februari 23 na 24 mwaka huu kupitia wingi wa madiwani wa Chama Cha Mapinduzi kiliazimia mradi huo kuhamishwa kutoka kata ya Chemchem na kupelekwa kata ya Ifucha kwa hoja dhaifu ya kusaidia watu wa kata za pembezoni.


Amebainisha kuwa mradi huo uliolengwa kutekelezwa kwenye zahanati ya Town Clinic ulilenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma ya afya ya mama na mtoto kwa wakazi wa kata sita ambazo ni Chemchem, Mwinyi, Kanyenye,Gongoni,Mbugani na Tambuka Reli katika Manispaa hiyo.


Diwani huyo ameeleza kuwa zahanati ya Town Clinic ni kongwe na iko kwenye kata yenye wakazi 14,453 wenye uwezo wa kufanya kazi ambao kimsingi wangenufaika na mradi huo ambao umehamishiwa kwenye kata ya Ifucha yenye wakazi 3,307 wenye uwezo wa kufanya kazi.


Kabata akifafanua zaidi amesema, “katika kipindi cha tarehe 18 Januari na tarehe 28 Februari mwaka huu katika zahanati hiyo akinamama 48 wamejifungulia hapo ukilinganisha na zahanati ya Ifucha katika kipindi hicho ilihudumia akinamama watatu kujifungua.”


Amefafanua kuwa katika kata ya Chemchem miongoni mwa watu wenye uwezo wa kufanya kazi wanawake ni 5,975 wakati katika kata ya Ifucha miongoni mwa watu wenye uwezo wa kufanya kazi wanawake ni 1,607.

Kabata amesema, “Zahanati ya Town Clinic kupitia mfuko wa bima ya Afya imeteuliwa kuwa kituo cha tiba kwa kadi (TIKA) na hivyo kuifanya kuhudumia akinamama wajawazito 32,988.”


Ameongeza, “katika mazingira hayo ni dhahiri kuwa wanasiasa wametumia nafasi zao vibaya kuwaumiza wananchi kwa maslahi ya kisiasa kuangalia uchaguzi wa mwaka 2020.”


Aidha katibu wa Chama Cha Wananchi CUF wilaya ya Tabora Kapasha H. Kapasha ameandika barua ya terehe 1 Machi mwaka huu kwenda kwa mkuu wa mkoa wa Tabora kumtaka kuingilia kati maazimio hayo ya baraza la madiwani.

No comments: