Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Saturday, March 26, 2016

MAOFISA WATENDAJI WAWILI WAPANDISHWA KIZIMBANI KWA RUSHWA



Na, Murugwa Thomas, Tabora.
Maofisa watendaji wawili wa kata na kijiji katika halmashauri ya wilaya ya Sikonge mkoani Tabora wamefikishwa mahakamani wakikabiliwa na mashitaka mawili ya kuomba na kupokea rushwa ya shilingi 700,000/=. 

Akiwasomea mashitaka mbele ya hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama ya wilaya ya Tabora Emanuel Ngigwana, wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU Edson Mapalala alisema watuhumiwa hao Alfred Mashaka afisa mtendaji wa kata ya Kiloleli na Thomas Dickson mtendaji wa kijiji cha Kanyamsenga walitenda makosa hayo Januari 4 mwaka huu.


Wakili huyo aliiambia mahakama hiyo kuwa katika shitaka la kwanza watuhumiwa  hao waliomba kiasi hicho cha fedha toka kwa Masuluzi Samweli ili wasimchukulie hatua za kisheria kwa kosa la kumpiga Mabula Sinyaka.


Mapalala aliongeza kuwa katika shitaka la pili watuhumiwa wakiwa ni watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Sikonge kwa pamoja walipokea shilingi 700,000/- toka kwa Masuluzi kama kishawishi na kushindwa kumchukulia hatua za kisheria.


Upande wa mashitaka kupitia kwa wakili Mapalala uliiambia mahakama hiyo kuwa upelelezi wa shauri hilo umekamilika na kuomba ipangwe tarehe nyingine kwa ajili ya kuanza usikilizwaji wa awali.


Watuhumiwa wote walikana mashitaka dhidi yao na wamepelekwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana kwa kutokuwa na watu wenye sifa hadi tarehe 29 Machi 2016 shauri hilo litakapoanza usikilizwaji wa awali.

No comments: