Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, March 27, 2016

MECHI YA TAIFA STARS NA CHAD YAOTA MBAWA




Timu ya Chad iliyokuwa icheze na timu ya taifa ya Tanzania “Taifa “Stars” kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Jumatatu Jioni,haitofika Tanzania baada ya kujitoa katika kuwania kufuzu fainali za Mataifa ya Afrika AFCON 2017 zitakazochezwa nchini Gabon.

Kwa mujibu wa barua iliyoandikwa Jumapili na katibu mkuu wa chama cha Soka nchini humo FTFA Moctar Mahamoud kwenda Shirikisho la Soka Barani Afrika CAF imeeleza kuwa Chad imeshindwa kufika Dar es Salaam kucheza mechi ya marudiano  kwa madai kuwa haina fedha za kuwawezesha kuendelea na mechi za kundi G.

Taifa hilo la Chad limejitoa baada ya kucheza mechi tatu za mzunguko wa kwanza, huku ikifungwa na timu zote, ambapo ikicheza ugenini ilifungwa na Nigeria bao 2 kwa 1,ikiwa kwenye ardhi ya nyumbani ikafungwa magoli 5 kwa 1 na Misri, na tarehe 23 mwezi huu ikashindwa kutamba mbele ya Tanzania baada ya kukubali kichapo cha bao 1 kwa bila ikiwa nyumbani.

Kwa hatua hiyo ya Chad,kundi G limebaki na timu tatu za Tanzania, Misri na Nigeria.

Kwa mujibu wa kanuni na taratibu za Shirikisho la Soka Barani Afrika CAF kujitoa kwa Chad kumesababisha kufutwa kwa matokeo yote ya timu hiyo, na hivyo kulifanya kundi G kuongozwa na Misri ikiwa na pointi 4 badala ya 7, Nigeria ya pili ikiwa na pointi 2 badala ya 5 na Tanzania inashika mkia ikiwa na pointi moja badala ya  4.

Aidha CAF imeitoza Chad faini ya dola za kimarekani 20,000 pamoja na kupigwa marufuku kushiriki hatua za kufuzu fainali za AFCON  mwaka 2019.

Hata hivyo Misri ikiwa nyumbani katika mji wa Alexandria wataikaribisha Nigeria katika mechi ya marudiano itakayochezwa Jumanne ya tarehe 29 mwezi huu baada ya mechi ya kwanza kuchezwa katika mji wa Kaduna na kutoka sare ya kufungana bao 1 kwa 1.


Kujitoa kwa Chad kumeyabakiza mataifa 50 ya Afrika yakiwania nafasi 15 za kufuzu fainali hizo za AFCON  ambapo zitaungana na mwenyeji Gabon na kukamilisha idadi ya timu 16.

Timu zitakazoongoza katika makundi yote 13 zitafuzu moja kwa moja kwenye fainali hizo na washindi wa pili wawili bora kutoka miongoni mwa makundi 12 ukiondoa kundi la kwanza lenye timu mwenyeji Gabon zitafuzu pia.


Hata hivyo Kamati ya Utendaji ya Shirikisho La Soka Barani Afrika CAF Mnamo tarehe 15 Januari,2015 ilipitisha uamuzi kwamba timu zikibaki tatu kwenye kundi ni timu moja tu ambayo itaoongoza kundi hilo ndio itafuzu fainali za AFCON.

Timu ya taifa ya Tanzania “Taifa Stars” itashuka kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam siku ya Jumamosi ya tarehe 4 Juni, 2016 kucheza na Misri.

No comments: