Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, March 27, 2016

WAKAZI WA KATA YA MWINYI MANISPAA YA TABORA WALALAMIKIA KUONDOLEWA KILOMETA NANE ZA MATENGENEZO YA BARABARA



Na Paul Christian, Tabora.

Wakazi wa kata ya Mwinyi katika Manispaa ya Tabora wamelilalamikia baraza la madiwani wa halmashauri ya Manispaa hiyo kwa hatua yake ya kupunguza kilometa nane kati ya kilometa kumi za barabara zilizotengewa bajeti ya matengenezo katika maeneo korofi katani humo.

Mmoja wa wakazi wa kata hiyo Martha Mwijalubi amesema kitendo hicho kimefanywa kwa makusudi ili kuwakomoa wakazi wa kata hiyo kwa kumchagua diwani kutoka Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA katika uchaguzi mkuu uliopita.

“Wingi wa madiwani wa chama tawala wameamua kuondoa kilometa hizo za barabara na kuzigawa katika kata nyingine ambapo barabara zao hazijaathiriwa sana na mvua zinazoendelea kunyesha.”Amebainisha mkazi huyo.

Alipohojiwa kuhusu suala hilo diwani wa kata hiyo Martin Mussa Daniel kwa tiketi ya CHADEMA amekiri kuwa  kikao cha baraza la madiwani kilichoketi tarehe 23 na 24 Februari mwaka huu kwa kutumia wingi wa madiwani wa Chama Cha Mapinduzi kilipitisha maazimio ya kuondoa kilometa nane za matengezo ya barabara katika kata hiyo na kubakisha kilometa mbili tu.

“Kama mwakilishi wa kata hiyo nilijitahidi kujenga hoja ya kutetea kilometa zote kumi zibaki kama ilivyopendekezwa kwa kuwa eneo la Mwinyi lina wakazi wengi na barabara zake zimekuwa zikiathiriwa mara kwa mara wakati wa msimu wa mvua.”Amesema diwani huyo.

Martin amebainisha kuwa ni dhahiri madiwani wa CCM walikuwa wamejipanga kufanya hivyo kwa lengo la kudhoofisha uwakilishi wa wananchi unaotokana na kumchagua mtu wa chama cha upinzani.

Ameongeza,“Hali hii itaathiri sana maendeleo ya Manispaa ya Tabora kwa kutumia itikadi za kisiasa na wingi wa madiwani wa CCM kupitisha maamuzi ya kukomoa wananchi wenye vyama na wasio na vyama kwa maslahi duni ya kisiasa yanayolenga uchaguzi wa mwaka 2020.”

No comments: