Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Saturday, March 19, 2016

NGOKO:"TASAF AWAMU YA TATU HAINA TAKWIMU SAHIHI YA WATOTO WANAOSTAHILI RUZUKU YA MASHARTI"



Na Paul Christian, Tabora.

Mpango wa kunusuru kaya masikini unaosimamiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF awamu ya tatu unakabiliwa na changamoto ya kutokuwa na takwimu sahihi ya idadi ya watoto wanaostahili kupata fedha za ruzuku ya masharti.

Mratibu wa TASAF mkoa wa Tabora Ngoko Buka amebainisha hayo wakati wa ziara ya kutembelea zoezi la kutoa fedha za ruzuku ya msingi na ya masharti kwa kaya masikini katika kata za Usoke,Ugalla na Uyumbu wilayani Urambo.

Amesema takwimu sahihi ya wanufaika wa ruzuku ya masharti inayotolewa kwa watoto wanaosoma shule za msingi na sekondari pamoja na wale wenye umri chini ya miaka mitano wanaohudhuria kliniki kutoka kaya masikini haijulikani kikamilifu kutokana na sababu mbalimbali.

Ngoko amezitaja sababu hizo kuwa ni pamoja na wakati wa zoezi la kuzitambua kaya masikini baadhi ya watoto waliandikishwa majina tofauti na yale wanayoyatumia shuleni hivyo kutoonekana kwenye madaftari ya mahudhurio katika shule husika.

Amesema sababu ya pili ni baadhi ya watoto kutoka kaya masikini kusoma kwenye shule za vijiji jirani tofauti na vijiji ambavyo kaya husika zinaishi hali ambayo imewafanya watoto hao kutokuwepo kwenye madaftari ya mahudhurio katika shule za vijiji wanavyoishi.

Mratibu huyo wa TASAF mkoa wa Tabora amesema kasoro hizo zimewafanya baadhi ya watoto kuondolewa kwenye orodha ya watoto wanaostahili kupata ruzuku ya masharti kwa madai ya kukiuka masharti kwa kutohudhuria masomo jambo ambalo sio sahihi.

Aidha Ngoko amebainisha kuwa katika shule za msingi na sekondari walimu wanapojaza fomu maalum za TASAF kuonyesha mwenendo wa mahudhurio hawana orodha ya wanafunzi wanaonufaika kutoka kaya masikini ambayo inaainisha idadi yao na madarasa wanayosoma.

Amesema ukosefu wa orodha ya wanafunzi kutoka kaya masikini inasababisha walimu kukabiliwa na ugumu wa kufanya rejea wakati wa ufuatiliaji wa mahudhurio ya wanafunzi hao hali ambayo imefanya kuwe na ugumu wa kupata takwimu za moja kwa moja katika shule hizo.

Mratibu huyo ameainisha kasoro nyingine iliyojitokeza ni walimu kulalamikia kutokuwa sehemu ya mpango wa kunusuru kaya masikini na badala yake wamekuwa wakitumika kama wajaza fomu za TASAF hali inayochangia kutowajibika ipasavyo.

Katika kukabiliana na changamoto hizo, Ngoko amewaagiza watendaji wa vijiji, walimu pamoja na wazazi au walezi wenye wanafunzi kutoka kaya masikini kukaa kwa pamoja na kuondoa kasoro zilizopo kwa kubaini majina sahihi ya wanafunzi na shule wanazosoma ili wanufaike na mpango kama ilivyokusudiwa.

No comments: