Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, March 6, 2016

SERIKALI YAITAKA JAMII KUCHUKUA TAHADHARI YA UGONJWA WA KIMETA



JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO


TAARIFA KWA UMMA


KUCHUKUA TAHADHARI KUHUSU UGONJWA WA KIMETA NA MAGONJWA MENGINE YATOKANAYO NA WANYAMA


UTANGULIZI

Wizara Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto inapenda kutoa taarifa kwa jamii kuchukua tahadhari ya magonjwa yanayoenezwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.

Magonjwa hayo ni kama kimeta, homa ya malale, tauni, homa ya bonde la ufa, kichaa cha mbwa, mafua makali ya ndege n.k.

Siku za karibuni ugonjwa wa Kimeta “Anthrax” ulitokea mkoani Kilimanjaro ambapo wagonjwa 23 waliugua. 

Ugonjwa huo uliripotiwa katika kijiji cha Rauya, kata ya Marangu Mashariki, wilaya ya Moshi Vijijini. 

Ugonjwa ulianza kwa mgonjwa mmoja aliyeugua baada ya kuchinja ng'ombe na mbuzi waliokuwa wamekufa. Mgonjwa huyu  alitibiwa katika hospital ya KCMC na kupona.

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi pamoja na timu ya Mkoa na Wilaya ilifanya uchunguzi na kubaini kuwa watu 23 waliugua na walihusika moja kwa moja katika uchinjaji au upishi wa nyama za ng'ombe wagonjwa au waliokufa, waligundulika kuwa na dalili za ugonjwa wa Kimeta.

Hatua zilizochukuliwa ni pamoja na:

Timu ya wataalamu wa afya kutoka ngazi ya Taifa walikwenda kushirikiana na timu ya mkoa na wilaya husika katika uchunguzi na udhibiti wa ugonjwa.

Ufuatiliaji wa waliokula nyama ya ng'ombe waliougua au kufa ulifanyika ambapo wote wamepata dawa za kinga, jumla ya watu 904 walihusishwa na kula nyama za ng'ombe waliokwishakufa (Wilaya ya Siha= 836, na Wilaya ya Moshi Vijijini=68)

Elimu ya afya kwa jamii jinsi ya kujikinga na ugonjwa huu Kunyunyuzia dawa ya kuua bakteria wanaoeneza ugonjwa katika maeneo ya kufugia au kuchinjia wanyama Kutoa elimu na kufanya ufuatiliaji wa mabucha yote ya nyama ambayo yanahusika na uuzaji wa nyama za ng'ombe waliokufa

     

Namna ya kuzuia Kimeta

Ugonjwa wa Kimeta unasababishwa na aina ya bakteria aitwaye “Bacillus anthracis” ambaye anashambulia wanyama mwitu, wafugwao pamoja na binadamu. 
Ugonjwa huo unaambukizwa kutoka mnyama kwenda kwa binadamu au kutoka binadamu mmoja kwenda mwingine au kwa njia ya:
       
·        kugusa nyama, damu na majimaji kutoka kwa mnyama au mwilini mwa mtu aliyeambukizwa ugonjwa huo.
·        kula  nyama ya mnyama aliye mgonjwa hasa ambayo haijaiva vizuri.
·        Kuvuta vumbi  lenye vimelea vilivyotoka kwa mnyama mgonjwa

Wizara inatoa rai kwa jamii kuchukua tahadhari za kujikinga na ugonjwa huu ambazo ni pamoja na:
       
·        Epuka kula nyama inayotokana na mnyama aliye mgonjwa au aliyekufa.

·        Tumia nyama iliyothibitishwa na mtaalamu wa mifugo.

·        Toa taarifa kwa wataalamu wa mifugo kuhusu wanyama wagonjwa au vifo vya wanyama.

·        Epuka kugusa nyama, damu au majimaji kutoka kwa mnyama au mwilini mwa mtu aliyeambukizwa ugonjwa huo bila vifaa kinga.

·        Epuka kula nyama ambayo haijaiva vizuri.

·        Toa chanjo kwa wanyama wafugwao.

Hitimisho

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto itaendelea kushirikiana na sekta ya mifugo na nyingine ili kuimarisha mikakati ya kudhibiti magojwa ya nayoenezwa kutoka kwa mifugo kwenda kwa binadamu kama magonjwa ya kimeta, homa ya malale, tauni, homa ya bonde la ufa, kiachaa cha mbwa, mafua makali ya ndege n.k. 

Jamii inaaswa kuzingatia maagizo yanayotolewa na wataalamu wa afya pamoja na wa mifugo ili kujikinga na magonjwa hayo na mara waonapo dalili za magonjwa hayo watoe taarifa mapema.

No comments: