Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, March 30, 2016

AFISA MTENDAJI WA KIJIJI APANDISHWA KIZIMBANI KWA KUOMBA NA KUPOKEA RUSHWA TSH 50,000/-




Na Thomas Murugwa, Tabora.

Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa TAKUKURU mkoani Tabora imemkamata na kumfikisha mahakamani afisa mtendaji wa kijiji Utimle wilayani Sikonge kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa ya shilingi elfu 50,000/-.

Akisoma mashitaka dhidi ya mshitakiwa huyo Batholomeo Athanas Sonda mbele ya hakimu wa mahakama ya mkoa wa Tabora Jackton Rushwela wakili wa TAKUKURU Edson Mapalala alisema mshitakiwa huyo alitenda kosa hilo mjini Sikonge kati ya tarehe mosi na pili Machi mwaka huu.

Wakili huyo wa TAKUKURU  alidai mahakamani hapo kuwa mtendaji huyo wa kijiji mnamo tarehe 1 Machi 2016  akiwa kwenye eneo la stendi ya mabasi ya Sikonge aliomba shilingi laki nne kutoka kwa Hussein Hamis Swalehe ili amruhusu aendelee kuvuna mazao ya misitu.

 Ilidaiwa katika shitaka la pili kuwa mtuhumiwa alipokea shilingi elfu 50,000/= toka kwa Swalehe ikiwa kama kishawishi ili amruhusu aendelee kuvuna mazao ya misitu bila kuwa na kibali toka kwa mkurugenzi wa maliasili.

 Mtendaji huyo amekana makosa yote mawili  na kesi hiyo impangwa kutajwa tarehe 5 Aprili 2016 ili ipangiwe tarehe ya usikilizwaji wa awali.

Hakimu Rushwela alikubali mtuhumiwa apewe dhamana ya watu wawili kwa ahadi ya shilingi milioni tano na kutoa masharti kwamba mmoja wa wadhamini awe ni mkazi wa manispaa ya Tabora ili iwe rahisi kumpata mtuhumiwa pindi anapohitajika.

Masharti hayo yamewekwa na mahakama kwa kile kilichodaiwa  kuwa watuhumiwa wengi wanapodhaminiwa na wakazi  wa nje ya manispaa ya Tabora wamekuwa wanashindwa kufika mahakamani na hivyo inakuwa ni vigumu kuwapata ili wajibu mashitaka yao.

Hii ni mara ya pili kwa watendaji wa vijiji vya wilaya ya Sikonge kufikishwa mahakamani mkoani hapa wakikabiliwa na mashitaka ya kuomba na kupokea rushwa katika kipindi kisichozidi wiki mbili.

Machi 23 mwaka huu  TAKUKURU iliwafikisha mahakamani Alfred Mashaka afisa mtendaji wa kata ya Kiloleli na Thomas Dickson afisa mtendaji wa kijiji cha Kanyamsenga kwa makosa ya kuomba na kupokea rushwa ya shilingi laki saba.

No comments: