Na Paul Christian, Tabora.
Mwanafunzi wa kike wa darasa la kwanza shule ya
msingi Kakurungu kata ya Milambo Itobo wilayani Nzega Asia Paulo amefariki
dunia baada ya kupigwa na radi.
Akizungumza na waandishi wa habari mtendaji wa
kata ya Milambo Itobo Raphael Bundala amesema tukio hilo limetokea Alhamis
mchana katika familia ya Ngelengi Makala katika kitongoji cha Mtakuja kijiji
cha Kakurungu katani humo.
Amesema wakati wa majira hayo ya mchana ilinyesha
mvua ya wastani iliyoambatana na radi ilipiga kwenye jiko la familia hiyo na kusababisha kifo cha mwanafunzi huyo
na kujeruhi watu wengine wanne.
Raphael amewataja watu waliojeruhiwa katika tukio
hilo kuwa ni Hadija Juma mwenye umri wa miaka 40 amejeruhiwa ubavuni na sehemu
ya paja, Sophia Ngelengi mwenye miaka 25 amejeruhiwa mbavuni,Salima Rashid
mwenye miaka 21 amejeruhiwa kwenye paji la uso na mtoto wa miaka 6 Abdalla
Ramadhan alipata majeraha miguuni.
Mtendaji huyo amefafanua kuwa majeruhi wote
walitibiwa katika zahanati ya Kakurungu na kuruhusiwa kurudi nyumbani.
No comments:
Post a Comment