Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Saturday, April 9, 2016

TAKUKURU YAGUNDUA MIANYA YA RUSHWA KWENYE MACHINJIO NA SOKO KUU MJINI TABORA


Na Paul Christian, Tabora.
  
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU mkoani Tabora imebaini uwepo wa mianya ya rushwa kwenye Machinjio na Soko kuu yanayosimamiwa na halmashauri ya manispaa ya Tabora.

Akizungumza na waandishi wa habari  Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Tabora Fidelis Kalungura amesema katika machinjio ya mjini Tabora taasisi hiyo iligundua ongezeko la viwango vya ushuru kwa shilingi 500 kwa kila ng’ombe anayehifadhiwa kwa siku zisizo za kazi.

Amesema pamoja na kutoza ushuru huo wenye maofisa wa halmashauri wanaosimamia machinjio hiyo wamekuwa hawatoi stakabadhi kwa wamiliki wa ng’ombe hao.

Kalungura amebainisha kuwa fedha hizo zinazokusanywa kupitia ushuru huo ambao hautolewi stakabadhi zimekuwa zikitumika kuwalipa malipo ya ziada watumishi hao wa umma.

Aidha amefafanua kwa mujibu wa sheria za nchi jukumu la kuwalipa malipo ya ziada watumishi hao ni la mwajiri wao ambaye ni mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya manispaa ya Tabora.

Kalungura amesema eneo jingine lililobainika kuwa na mianya ya rushwa ni ukarabati mdogo wa machinjio hiyo ambao haukulingana na thamani ya halisi ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya kazi hiyo.

Mkuu huyo wa TAKUKURU mkoa wa Tabora amesema mwanya mwingine wa rushwa katika machinjio hiyo upo kwenye usimamizi wa Sheria, Kanuni na taratibu kwa kuruhusu magari yasiyo na ubora kubeba nyama kwenda kwa walaji.

Amebainisha kuwa katika eneo hilo  kutokana na udhaifu wa usimamizi wa sheria baiskeli na pikipiki zimeruhusiwa kusafirisha nyama jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

Kalungura amesema taasisi hiyo imebaini mianya ya rushwa kwenye Soko kuu la mjini Tabora kwa kutofahamika idadi ya walipa ushuru kwa kuwa idadi kamili ya vizimba haipowazi.

Aidha ameeleza katika soko hilo kunaukiukwaji wa sheria,kanuni na taratibu kwa kuwa ushuru haulipwi kwa wakati na hakuna hatua zozote zinazochukuliwa.

Mkuu huyo wa TAKUKURU amesema taasisi yake imebaini kuwa wakusanya ushuru hawalipwi posho zao za kazi za ziada kwa wakati na wanaidai halmashauri ya Manispaa ya Tabora jambo ambalo linatoaushawishi wa kupokea rushwa.

Kalungura amebainisha katika soko hilo hakuna mfumo unaokubalika katika utunzaji wa kumbukumbu na ufuatiliaji pia hakuna ushirikishwaji wa wafanyabiashara katika kufanya maamuzi mbalimbali yanayowahusu.

Ameeleza kuwa wakusanya ushuru hao wanakabiliwa na ukosefu wa vitendea kazi hawana kompyuta kwa ajili ya kutunzia kumbukumbu wala vyombo vya usafiri kama baiskeli na pikipiki.

Hata hivyo taasisi hiyo imeiagiza halmashauri ya manispaa ya Tabora kuchukua hatua za kuziba mianya hiyo ya rushwa katika Machinjio na Soko Kuu mjini Tabora.



No comments: