Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Wednesday, April 27, 2016

UKATAJI MITI UNAHATARISHA HALI YA HEWA YA MKOA WA TABORA



Na Hastin Liumba,Tabora 

Diwani wa kata ya Gongoni manispaa ya Tabora Kessy Sharrif Abdulrahman amewaasa wakazi wa kata hiyo na maeneo mengine kuzitumia mvua zinazoendelea kunyesha kwa kupanda miti.

Amesema suala la kupanda miti linapaswa kuwa ajenda ya kudumu kwa wakazi wa mkoa wa Tabora ambao kwa sasa umeanza kuathiriwa na vitendo vya uharibifu wa mazingira ikiwemo ukataji miti kwa matumizi mbalimbali.

Abdulrahman amebainisha kuwa maeneo ya mkoa wa Tabora kwa sasa yameanza kukabiliwa na uhaba wa mvua na ongezeko la joto tofauti na miaka iliyopita.

Katika kutekeleza azma yake kwa vitendo diwani huyo wa kata ya Gongoni amekuwa akiitumia siku ya Jumamosi ya kila mwisho wa mwezi kupanda miti na kufanya usafi katika kata yake.

Amesema hatua hiyo inalengo la kuongeza kasi ya kupanda miti pamoja na kuhakikisha miti hiyo inatunzwa ipasavyo na kila mkazi wa kata hiyo.
Abdulrahman ameeleza kuwa kitendo cha kupanda miti mara kwa mara kitasaidia kizazi kinachochipukia kujenga utamaduni wa kuthamini miti ili kuhifadhi na kulinda mazingira.

Diwani huyo amesema suala la ukataji miti kiholela limesababishwa na shughuli za binadamu ikiwemo kuchoma mkaa,kuni, upasuaji mbao, kilimo cha tumbaku na mazao mchanganyiko, ufugaji na ujenzi wa makazi.

Aidha amesema kilimo cha kuhama hama,maarifa madogo ya sayansi ya udongo pamoja na ukosefu wa maarifa ya kilimo cha kisasa ni miongoni mwa sababu zinazopelekea ukataji wa miti ili kupata maeneo makubwa ya kulima au kufuga.

Abdulrahman amefafanua kuwa licha ya wakulima wengi kulima maeneo makubwa wamekuwa wakivuna kiasi kidogo cha mazao ukilinganisha na muda,nguvu na rasilimali zingine walizotumia.

Diwani huyo wa kata ya Gongoni ameishauri serikali kuwekeza katika matumizi ya nishati mbadala kwa maeneo ya mijini na vijijini, kutoa maarifa chanya ya kilimo na ufugaji bora pamoja na kuhimiza jamii kupanda miti kwa wingi na kuitunza.

Amesema mradi huo wa upandaji miti ameubuni yeye mwenyewe na kwamba atawashirikisha zaidi vijana ili waweze kuwekeza nguvu na maarifa yao katika kutunza mazingira.

Wednesday, April 20, 2016

MARTIN JOL ATANGAZA KIKOSI CHA AL AHLY KITAKACHOIMALIZA YANGA LEO



JOL
Meneja wa timu ya Al Ahly “Red devils” ya nchini Misri Martin Jol ametangaza kikosi cha wachezaji 11 kitakachoivaa Yanga ya Tanzania katika mechi ya marudiano ya ligi ya Mabingwa barani Afrika itakayochezwa majira ya saa 19:30 kwa saa za Misri.



Mechi hiyo ya hatua ya 16 bora itachezwa leo Jumatano kwenye uwanja wa Borg El-Arab katika mji wa Alexandria.



Meneja huyo Martin Jol ametangaza kikosi hicho kuwa na wachezaji ambao ni Sherif Ekramy;Ahmed Fathi,Rami Rabia,Ahmed Hegazy,Sabry Rahil;Hossam Ashour;Hossam Ghaly;Abdallah El-Said,Momen Zakaria,Ramadan Sobhy na Amr Gamal.



Katika mechi ya kwanza iliyochezwa jijini Dar es Salaam timu hizo zilitoka sare ya bao 1 kwa 1.



Martin Jol ni mholanzi mwenye umri wa miaka 60 ni kocha wa zamani wa ligi kuu ya Uingereza ambapo amewahi kuzinoa timu za Tottenham Hotspur na Fulham.



Kocha huyo pia amewahi kuifundisha klabu ya Ajax Amsterdam ya Uholanzi na Humburger SV ya Ujerumani.



Hans van der Pluijm ni kocha wa klabu ya Yanga ya Tanzania amezaliwa tarehe 3 Januari, 1943 katika eneo la Nieuwkuijk, nchini Uholanzi.

Amewahi kuzifundisha timu kadhaa ikiwemo FC Den Bosch na amekuwa nchini Ghana tangu mwaka 1999.


Kabla ya kujiunga na Yanga amewahi kuzifundisha timu za Medeama SC,  Berekum Chelsea ambapo kwa timu za Heart of Lions na  Ashanti Gold amezinoa kwa misimu tofauti.

TAKUKURU YAMHOJI RAIA WA VIETNAM KWA TUHUMA ZA RUSHWA.



Na, Thomas Murugwa,Tabora.

Mkuu wa kitengo cha biashara cha kampuni ya simu za mkononi mtandao wa Hallotel  Hoang Vanch Linh (36) maarufu kwa jina la “Peter”  amekamatwa na kuhojiwa  na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa  - TAKUKURU  kwa tuhuma za kuomba na kupokea rushwa.

Akizungumza na waandishi wa habari  kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Tabora Fidelis Kalungura amesema raia huyo  wa Vietnam alikamatwa  Aprili 08 mwaka huu baada ya maofisa wake kupewa taarifa na kisha kuweka mtego uliomnasa.

Kamanda Kalungura amesema kuwa raia huyo wa Vietnam alikamatwa akipokea rushwa ya shilingi laki tano  ikiwa ni sehemu ya malipo ya shilingi milioni 1.5 alizoomba kutoka kampuni ya ulinzi iitwayo State.

Amebainisha kuwa TAKUKURU ilipewa taarifa kuwa mkuu huyo wa kitengo cha biashara Hallotel aliomba apewe fedha hizo  toka kwenye kampuni hiyo iliyopewa kazi ya kulinda minara ya simu ili waendelee kupewa mkataba wa kazi hiyo.

Kalungura amesema kwamba  mara baada ya kukamatwa na kuhojiwa  Mvietinam huyo alikana na alipewa dhamana wakati uchunguzi zaidi ukiendelea.

Kamanda Kalungura amebainisha kuwa bado wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo  na endapo ikibainika kama aliomba na kupokea fedha hizo kama hongo atafikishwa mahakamani .

MAHAKAMA YATUPILIA MBALI KESI YA KUPINGA MATOKEO YA DIWANI WA CHADEMA





NA Thomas Murugwa,Tabora.

Mahakama ya hakimu mkazi mfawidhi wa wilaya ya Tabora imetupilia mbali maombi  ya Julius Salawe wa CCM aliyetaka kutenguliwa  kwa ushindi wa udiwani wa Machibya Emmanuel  wa CHADEMA katika kata ya Ugembe wilayani Nzega.

Akisoma hukumu hiyo hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama hiyo Emanuel Ngigwana amesema mlalamikaji ameshindwa kuthibitisha pasipo shaka  maombi yake yote matano ili mahakama itengue matokeo yaliyompa ushindi mgombea huyo wa CHADEMA.

Amesema kuwa  mlalamikaji alishindwa kuleta ushahidi  wa kuunga mkono madai yake ikiwemo kujaza fomu za malalamiko  ya kupinga matokeo ya vituo husika hata kupitia kwa mawakala wake.

Hakimu huyo ameeleza kuwa  katika kesi za uchaguzi,mlalamikaji amepewa jukumu  la kuthibitisha pasipo shaka yoyote madai yake dhidi ya mlalamikiwa jambo ambalo mlalamikaji katika shauri hilo ameshindwa kufanya hivyo.

Pamoja na kutupilia mbali madai hayo mahakama ilimthibitisha Machibya
wa CHADEMA kuwa diwani halali wa kata hiyo na  imemtaka mlalamikaji huyo Julius Salawe alipe gharama za uendeshaji wa shauri hilo.

Mahakama hiyo pia  imetubilia  mbali madai ya Suleiman Denis Onesmo wa CHADEMA aliyetaka kutenguliwa kwa ushindi wa diwani wa kata ya
Silambo,Wilayani Kaliua Ibrahim Issaya Kifoka wa CCM na kumthibitisha yeye kuwa diwani halali.

Hakimu Ngigwana katika uamuzi wake uliochukua  saa mbili amesema
Mlalamikaji ameshindwa kuithibitishia mahakama pasipo shaka madai yake kwa kuleta ushahidi hafifu ulioshindwa kutengua ushindi wa Kifoka.

Akisoma uamuzi  huo hakimu Ngigwana amesema madai kuwa mlalamikiwa wa kwanza  Kifoka alipeleka kura bandia 68 katika  moja ya kituo cha kupigia kura hayakuthibitishwa na mlalamikaji kwani kura hizo bandia hazikuwasilishwa  mahakamani hapo kama kielelezo.

Hakimu huyo amesema kwa ufupi mlalamikaji hakuwa na ushahidi
wenye nguvu huku ushahidi wake ukiwa ni wa kusikia na kuelezwa na watu akiwemo wakala wake.

katika madai Kwamba mlalamikiwa alimtumia  mtoto  wake Issaya Kifoka
kumsimamia, mahakama ameona kuwa  hilo halijathibitishwa na upande wa mlalamikaji kama ni kosa kwani hata mdai  alimtumia ndugu yake Paul Dennis kuwa wakala.

Kutokana na kitendo cha mlalamikaji kushindwa kuthibisha madai yake
mahakama ilimthibitisha Ibrahim  Kifoka kuwa diwani halali wa kata ya
Silambo na kuwataka wahusika kuendelea kuishi kwa amani kwani baada ya uchaguzi maisha lazima yaendelee.



Wednesday, April 13, 2016

LIGI KUU TANZANIA BARA: "KADI NYEKUNDU NI KWA YANGA TU"




Mechi ya jana ya ligi kuu Soka Tanzania Bara kati ya Yanga na Mwadui FC kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam,Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 2 kwa 1 na kufikisha pointi 56 kwa michezo 23 ikiwa nyuma ya Simba iliyoko kileleni yenye pointi 57 baada ya kucheza mechi 24.

Mwamuzi wa kati wa mechi hiyo Selemani Kinugani alimtoa kwa kadi nyekundu, Iddi Mobby kunako dakika ya 70 ya mchezo kwa kumchezea rafu kiungo wa Yanga, Thabani Kamusoko.

Mshambuliaji hatari wa Yanga, Mzimbabwe, Donald Ngoma  ameibua mjadala mpya kwa mabeki wa timu za Ligi Kuu Tanzania Bara kwa kupata kadi nyekundu.

Ngoma ambaye ameifungia Yanga mabao 14, mpaka sasa kwenye ligi kuu ameweka rekodi mpya ya kuwasababishia mabeki wa kati watatu kadi nyekundu kila alipokutana nao kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika michezo mitatu ya Yanga iliyopigwa kwenye uwanja huo dhidi ya Mbeya City, Simba SC na Kagera Sugar yote ilimalizika kwa timu hizo kuwa na wachezaji pungufu kutokana na kadi nyekundu zilizosababishwa na Ngoma.

Katika mechi yao na Mbeya City, Tumba Sued alipigwa kadi nyekundu baada ya kugongana na Ngoma katika dakika ya 56 na kusababisha pengo kwa timu hiyo ambapo mwisho wa matokeo Yanga ilishinda 3-0.

Mechi Yanga dhidi ya Simba iliyochezwa Februari 21 mwaka huu, kunako dakika ya 24 ya mchezo Mwamuzi wa kati Jonesia Rukyaa alimtoa nje ya dimba  kwa kadi nyekundu beki wa wekundu hao, Abdi Banda kwa kumchezea rafu Ngoma. Katika mechi hiyo Yanga ikashinda kwa magoli 2 kwa bila .

Ngoma kwa mara nyingine alisababisha kwa Kagera Sugar ambapo beki wao, Shaban Ibrahim Sunza, alitolewa nje kwa kadi nyekundu baada ya kuzawadiwa njano mbili kutokana na kumchezea kibabe . Mechi hiyo pia Yanga ilishinda 3-1.

Timu ya Mbeya City imewahi kulalamika kuwa kila inapokutana na Yanga wachezaji wake wamekuwa wakitolewa kwa kadi nyekundu.

Katibu mkuu wa Klabu hiyo Emmanuel Kimbe amewahi kusema timu hiyo katika msimu wao wa kwanza ligi kuu Tanzania Bara 2013/2014 walipokutana na Yanga kadi nyekundu ilikwenda kwa mchezaji wao Steven Mazanda.

Amesema msimu wao wa pili wa 2014/2015 walipokutana na Yanga kadi nyekundu ilienda kwa Them Felix.

Na msimu wao wa tatu wa 2015/2016 wameshuhudia jambo lile lile likijirudia.