Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Friday, July 1, 2016

MWANRI:AZIGIZA HALMASHAURI KUTENGA ASILIMIA TANO YA MAPATO YA NDANI KWA AJILI YA VIJANA



Na Paul Christian,Tabora

Halmashauri za wilaya na Manispaa mkoani Tabora zimeagizwa kutenga asilimia tano ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya kuwakopesha vijana katika maeneo yao.

Mkuu wa mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri ametoa agizo hilo jana alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tano ya kutambua fursa za ajira kwa vijana 191 wa wilaya ya Uyui yaliyofanyika katika chuo cha kilimo Tumbi katika manispaa ya Tabora.

“Ninaanza kucheck mahesabu ya halmashauri zote za mkoa wa Tabora na nikibaini halmashauri ambayo haijatenga asilimia tano kwa ajili ya vijana hatutapitisha bajeti ya halmashauri husika,” amesema.

Mwanri amesisitiza kuwa suala la kutenga asilimia tano ya mapato ya ndani ya halmashauri hizo ni la kisheria na kwamba halina mjadala.

Aidha amezitaka halmashauri hizo kuweka vipaumbele madhubuti katika mipango yao ili ziweze kuondoa vikwazo vinavyoweza kuwakwamisha vijana kujichukulia fursa mbalimbali za kiuchumi.

“Halmashauri zinapaswa kuweka vipaumbele katika kuchimba mabwawa, kutengeneza miundombinu ya barabara pamoja na mambo mengine kwa lengo la kuwafanya vijana wanaojiajiri wayafikie masoko na kutoa huduma mbalimbali za kibiashara.”Amesema Mwanri.

Mkuu huyo wa mkoa amezitaka halmashauri hizo kutengeneza mazingira wezeshi kwa vijana ili wawe wabunifu wa kujiajiri na kutoa ajira kwa watu wengine.

Akitoa rai kwa vijana hao amesema wanapaswa kubadili mtazamo wa kutaka kuajiriwa na badala yake wafikirie kuwa waajiri wa wale wanaofikiria kuhitimu masomo na kuajiriwa.

Awali kiongozi wa shirika la Millenium Promise Tanzania Dkt. Gerson Nyadzi amesema mafunzo hayo yanatokana na mradi unaojulikana Opportunities for Youth Employment (OYE).

“Vijana hawa wamejifunza nini maana ya mawasiliano,kuwa na nia au malengo katika maisha yao,kuweka kumbukumbu na kuhesabu,namna ya kupunguza msongo (stress management) pamoja na mawasiliano na utambuzi wa fursa.” Amesema.

Amesema mafunzo hayo ni ya awali yanayojulikana kama “stadi za kijamii” na hatua itakayofuata itakuwa ni kufundishwa masuala ya utaalam au ufundi (technical skills training).

Nyadzi amebainisha kuwa katika mafunzo hayo ya awali vijana hao wamejifunza kwa kujigawa katika makundi makuu matatu ikiwemo kilimo cha bustani,ufugaji wa kuku na nyuki.

Ameyataja makundi mengine kuwa ni kutafuta nishati mbadala (renewable energy) ambapo watafanya biogas na utengenezaji wa majiko banifu pamoja na kundi la usafi wa mazingira na maji ( water sanitation and hygiene).

Dkt. Nyadzi amesema vijana hao wenye umri wa kati ya miaka 18 na 30 wanatoka katika kata za Magiri,Ilolangulu,Kigwa,Isila na Isikizya katika wilaya ya Uyui na kwamba walilengwa vijana 210 lakini waliofika na kupata mafunzo hayo ni vijana 191.

Naye mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Uyui Said Ntahondi amemuomba mkuu huyo wa mkoa kuyataka makampuni yanayonunua zao la tumbaku mkoani Tabora kuwatumia vijana hao kupanda miti na shughuli nyingine zinazotokana na zao hilo badala ya kuchukua watu wengine.



No comments: