Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Sunday, July 17, 2016

TANROADS KUSHIRIKISHA SERIKALI ZA VIJIJI KUBAINI MAENEO KOROFI



Na Paul Christian,Tabora.

Wakala wa Barabara nchini (TANROADS) mkoa wa Tabora wamepongezwa kwa kutengeneza barabara yenye urefu wa kilometa 46.6 kutoka Ulyankulu hadi Ng’wande ambayo ilikuwa haipitiki wakati wa mvua za masika.

Akiwahutubia wakazi wa vijiji vya Taba,Sasu na Kashishi vilivyopo wilaya ya Kaliua Mbunge wa Jimbo la Ulyankulu John Peter Kadutu alisema TANROADS mkoa wa Tabora wamefanya kazi nzuri iliyorudisha matumaini ya wakazi hao kuweza kuyafikia maeneo mengine.

Alisema, “Barabara hii ni uti wa mgongo wa mawasiliano ya kiuchumi kati ya wakazi wa jimbo la Ulyankulu upande wa mkoa wa Tabora pamoja na Ushetu na Kahama kwa upande wa mkoa wa Shinyanga.”

Kadutu alifafanua kuwa TANROADS pia wamepanga kuimarisha barabara ya kutoka Makazi kupitia Uyowa hadi makao makuu ya wilaya, Kaliua ambapo hakukuwa na barabara ya uhakika kuunganisha maeneo hayo.

Akizungumzia barabara hiyo mmoja wa wakazi wa kijiji cha Taba Yudita Sayumwa  alishauri, “Wataalam wa TANROADS wanapaswa kuwauliza wenyeji kuhusu maeneo korofi ambayo hukatika wakati wa mvua ili yafanyiwe matengenezo ya uhakika tofauti na ilivyosasa.”

Kaimu afisa mtendaji wa kijiji cha Sasu Samwel Gogoja Ngokolo naye alitoa ushauri kwa meneja wa TANROADS mkoa wa Tabora kuhusisha serikali za vijiji ili kubaini maeneo korofi pamoja na kuweka matuta kudhibiti mwendokasi wa magari eneo la shule ya msingi kijijini humo.

Kwa upande wake mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Kagera kata ya Kashishi jimboni humo Dennis Steven Mkindo alitaka ufafanuzi kuhusu baadhi ya matengenezo katika barabara hiyo kuonekana dhaifu kwa kuwa haijawekwa molamu.

Akijibu hoja hizo mhandisi wa TANROADS mkoa wa Tabora anayeshughulikia barabara za mkoani humo Siperi Kato alisema, “kazi ya kujenga karavati bado inaendelea na mkandarasi bado hajamaliza kazi.”

Alibainisha kuwa mkandarasi huyo bado anayomakaravati karibu ya 100 na kwamba amekuwa akiyaanda kwa ajili ya kudhibiti maeneo korofi katika barabara hiyo.

Mhandisi Kato aliongeza, “TANROADS kwa kushirikiana na mkandarasi kampuni ya SAMOTA watahusisha viongozi wa serikali za vijiji hivyo ili kubaini maeneo yanayohitaji matengenezo ya ziada kutoka na uzoefu wao.”

Mhandisi huyo alitoa ushauri kwa wakazi wa vijiji hivyo kuzingitia umbali wa hifadhi ya barabara kwa kupima mita 30 kutoka katikati ili kujenga makazi au maeneo ya biashara kwa kuwa imepandishwa hadhi na kuwa ya mkoa tofauti na zamani.

No comments: