Featured Post

KITUMBO:MAWASILIANO MADHUBUTI YA KIUTAWALA NI SIRI YA MAFANIKIO

Na Paul Christian, Tabora. Mawasiliano mazuri ya kiutawala baina ya wenyeviti na watendaji wa mitaa na wananchi ni jambo muhimu kat...

Saturday, June 4, 2016

MWANRI: AAGIZA MGOGORO WA KIWANJA CHA TBC UMALIZWE NDANI YA WIKI TATU



Na Hastin Liumba,Tabora

MKUU wa mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri ametoa wiki tatu kwa mkurugenzi wa halmashauri ya manispaa Tabora Sipola Liana kuhakikisha mgogoro wa kiwanja kati ya shirika la utangazaji Tanzania TBC, halmashauri hiyo na wananchi unapatiwa utatuzi.

Agizo hilo amelitoa kwenye kikao cha maalumu cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo wakati wa kuchangia na kujadili taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali CAG kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015.

Mkuu huyo wa mkoa amesema amefuatilia nyaraka za TBC na kugundua kiwanja hicho ni mali ya shirika hilo, hivyo wananchi wanaoendelea kujenga katika kiwanja hicho ni wavamizi na waondolewe.

"Natoa wiki tatu kwako mkurugenzi kuhakikisha mgogoro wa kiwanja cha TBC unamalizwa na nipewe taarifa kabla ya kuchukua hatua."alisisitiza.

Mwanri amesema jambo hilo liko wazi lakini anashangazwa na uongozi wa manispaa kushindwa kuchukua hatua.

"Nilichogundua kuna udhaifu wa kiuongozi na idara ya ardhi kuna ubabaishaji wa hali ya juu, ni lazima tuchukue hatua dhidi ya wahusika."ameonya.

Amefafanua haiwezekani kiwanja kimoja kinatolewa kwa watu wawili na kupelekea mgogoro baina yao.

Amesema amepokea malalamiko mengi kutoka kwa wananchi wakimueleza Manispaa Tabora kushindwa kumaliza matatizo hayo.

Amesema yeye ni mwakilishiwa Rais hivyo asingependa kuona katika mkoa wake watendaji wanaofanya kazi kwa mazoea na kwamba wanaacha mara moja.

Katika hatua nyingine baraza la madiwani la manispaa hiyo lilipitisha azimio la kuwasimamisha kazi watumishi wanne wa idara ya ardhi ili kupisha uchunguzi juu ya tuhuma mbalimbali zinazoikabili idara hiyo.

Watumishi hao waliosimamishwa ni Mohammed Matola,Stanley Yungi,Lazaro Iragila na Allan Mbato ambao wanatuhumiwa na wananchi katika suala zima la viwanja manispaa Tabora.

Hatua hiyo ni ya pili kuchukuliwa na baraza hilo la madiwani ambapo kwa mara ya kwanza iliwasimamisha kazi watumishi watano wa idara hiyo lakini walirejeshwa kazini mamlaka za juu za serikali.

No comments: